0:00
0:00

Mlango 1

Bwana akanena na Musa katika bara ya Sinai, hemani mwa kukutania, siku ya kwanza ya mwezi wa pili, katika mwaka wa pili baada ya kutoka kwao nchi ya Misri, akamwambia,
2 Fanyeni hesabu ya mkutano wote wa wana wa Israeli, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina ilivyo, kila mtu mume kichwa kwa kichwa;
3 tangu mwenye miaka ishirini umri wake, na zaidi, wote wawezao kutoka kwenenda vitani katika Israeli; wewe na Haruni mtawahesabu kwa kuandama majeshi yao.
4 Tena mtu mume mmoja wa kila kabila atakuwa pamoja nanyi; kila mmoja aliye kichwa cha nyumba ya baba zake.
5 Na majina ya hao waume watakaosimama pamoja nanyi ni haya; Wa Reubeni; Elisuri mwana wa Shedeuri.
6 Wa Simeoni; Shelumieli mwana wa Suri-shadai.
7 Wa Yuda; Nashoni mwana wa Aminadabu.
8 Wa Isakari; Nethaneli mwana wa Suari.
9 Wa Zabuloni; Eliabu mwana wa Heloni.
10 Katika wana wa Yusufu; wa Efraimu, Elishama mwana wa Amihudi; na wa Manase; Gamalieli mwana wa Pedasuri.
11 Wa Benyamini Abidani mwana wa Gideoni.
12 Wa Dani; Ahiezeri mwana wa Amishadai.
13 Wa Asheri; Pagieli mwana wa Okirani.
14 Wa Gadi; Eliasafu mwana wa Deueli.
15 Wa Naftali; Ahira mwana wa Enani.
16 Hao ndio walioitwa wa mkutano, wakuu wa kabila za baba zao; nao ndio vichwa vya wale maelfu ya Israeli.
17 Basi Musa na Haruni wakawatwaa hao watu waume waliotajwa majina yao;
18 nao waliukutanisha mkutano mzima, siku ya kwanza ya mwezi wa pili, nao wakaonyesha ukoo wa vizazi vyao kwa kuandama jamaa zao, kwa nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, kichwa kwa kichwa.
19 Kama Bwana alivyomwagiza Musa, ndivyo alivyowahesabu huko katika bara ya Sinai.
20 Na wana wa Reubeni, mzaliwa wa kwanza wa Israeli, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, kichwa kwa kichwa, kila mtu mume tangu umri wa miaka ishirini na zaidi wote walioweza kwenda vitani;
21 wale waliohesabiwa katika kabila ya Reubeni, walikuwa watu arobaini na sita elfu na mia tano (46,500).
22 Katika wana wa Simeoni, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, wale waliohesabiwa kama hesabu ya majina, kichwa kwa kichwa, kila mume tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani;
23 wale waliohesabiwa katika kabila ya Simeoni, walikuwa watu hamsini na kenda elfu na mia tatu (59,300).
24 Katika wana wa Gadi, kwa kuandama vizazi vyao, jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani;
25 wale waliohesabiwa katika kabila ya Gadi, walikuwa watu arobaini na tano elfu na mia sita na hamsini (45,650).
26 Katika wana wa Yuda, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani;
27 wale waliohesabiwa katika kabila ya Yuda, walikuwa watu sabini na nne elfu na mia sita (74,600).
28 Katika wana wa Isakari, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kwa hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani;
29 wale waliohesabiwa katika kabila ya Isakari, walikuwa watu hamsini na nne elfu na mia nne (54,400).
30 Katika wana wa Zabuloni, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani;
31 wale waliohesabiwa katika kabila ya Zabuloni, walikuwa watu hamsini na saba elfu na mia nne (57,400).
32 Katika wana wa Yusufu, maana katika wana wa Efraimu, vizazi vyao kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani,
33 wale waliohesabiwa katika kabila ya Efraimu, walikuwa watu arobaini elfu na mia tano (40,500).
34 Katika wana wa Manase, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani;
35 wale waliohesabiwa katika kabila ya Manase, walikuwa watu thelathini na mbili elfu na mia mbili (32,200).
36 Katika wana wa Benyamini, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani;
37 wale waliohesabiwa katika kabila ya Benyamini, walikuwa watu thelathini na tano elfu na mia nne (35,400).
38 Katika wana wa Dani, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani;
39 wale waliohesabiwa katika kabila ya Dani, walikuwa watu sitini na mbili elfu na mia saba (62,700).
40 Katika wana wa Asheri, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani;
41 wale waliohesabiwa katika kabila ya Asheri, walikuwa watu arobaini na moja elfu na mia tano (41,500).
42 Katika wana wa Naftali, vizazi vyao, kwa kuandama jamaa zao, na nyumba za baba zao, kama hesabu ya majina, tangu umri wa miaka ishirini na zaidi, wote walioweza kwenda vitani;
43 wale waliohesabiwa katika kabila ya Naftali, walikuwa watu hamsini na tatu elfu na mia nne (53,400).
44 Hao ndio waliohesabiwa, ambao Musa na Haruni na wale wakuu wa Israeli watu kumi na wawili waliwahesabu; walikuwa kila mmoja kwa ajili ya nyumba ya baba zake.
45 Basi hao wote waliohesabiwa katika wana wa israeli kwa kuandama nyumba za baba zao tangu umri wa miaka ishirini na zaidi; wote walioweza kwenda vitani katika Israeli;
46 hao wote waliohesabiwa walikuwa ni watu waume mia sita na tatu elfu na mia tano na hamsini (603,550).
47 Lakini Walawi kwa kuiandama kabila ya baba zao hawakuhesabiwa katika watu hao.
48 Kwa kuwa Bwana alinena na Musa, na kumwambia,
49 Hiyo kabila ya Lawi tu usiihesabu, wala usiitie hesabu yao katika wana wa Israeli;
50 lakini uwaweke Walawi wawe juu ya maskani ya ushahidi, na juu ya vyombo vyake vyote, na juu ya vitu vyake vyote; wao wataichukua hiyo maskani, na vyombo vyake vyote; nao wataitumikia, na kupanga hema zao kwa kuizunguka maskani pande zote.
51 Tena hapo maskani itakapokwenda mbele, Walawi wataishusha; tena hapo maskani itakaposimamishwa, Walawi wataisimamisha; na mgeni atakayekaribia atauawa.
52 Na wana wa Israeli watazipanga hema zao, kila mtu katika marago yake mwenyewe, kila mtu hapo ilipo beramu yake mwenyewe, kama majeshi yao yalivyo.
53 Lakini Walawi watapanga hema zao kuizunguka maskani ya ushahidi pande zote, ili zisiwe hasira juu ya mkutano wa wana wa Israeli; kisha Walawi wataulinda ulinzi wa hiyo maskani ya ushahidi.
54 Ndivyo walivyofanya wana wa Israeli; kama yote Bwana aliyomwagiza Musa, ndivyo walivyofanya.