0:00
0:00

Mlango 2

Bwana akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia,
2 Wana wa Israeli watapanga kila mtu penye beramu yake mwenyewe, na alama za nyumba za baba zao; kuikabili hema ya kukutania ndiko watakakopanga kwa kuizunguka pande zote.
3 Na hao watakaopanga upande wa mashariki, kwa kuelekea maawio ya jua, ndio wale wa beramu ya marago ya Yuda, kwa majeshi yao; na mkuu wa wana wa Yuda atakuwa Nashoni mwana wa Aminadabu.
4 Na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa sabini na nne elfu na mia sita.
5 Na hao watakaopanga karibu naye ni kabila ya Isakari; na mkuu wa wana wa Isakari atakuwa Nethaneli mwana wa Suari;
6 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa hamsini na nne elfu na mia nne;
7 na kabila ya Zabuloni; na mkuu wa wana wa Zabuloni atakuwa Eliabu mwana wa Heloni;
8 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa hamsini na saba elfu na mia nne.
9 Hao wote waliohesabiwa katika marago ya Yuda walikuwa mia na themanini na sita elfu na mia nne, kwa majeshi yao. Hao ndio watakaosafiri mbele.
10 Upande wa kusini kutakuwa na beramu ya marago ya Reubeni kwa majeshi yao; na mkuu wa wana wa Reubeni atakuwa Elisuri mwana wa Shedeuri.
11 Na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa arobaini na sita elfu na mia tano.
12 Na hao watakaopanga karibu naye ni kabila ya Simeoni; na mkuu wa wana wa Simeoni atakuwa Shelumieli mwana wa Suri-shadai;
13 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa hamsini na kenda elfu na mia tatu;
14 na kabila ya Gadi; na mkuu wa wana wa Gadi atakuwa Eliasafu mwana wa Deueli;
15 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa arobaini na tano elfu na mia sita na hamsini.
16 Wote waliohesabiwa katika marago ya Reubeni walikuwa mia na hamsini na moja elfu na mia nne na hamsini, kwa majeshi yao. Nao ndio watakaosafiri mahali pa pili.
17 Ndipo hema ya kukutania itasafiri, pamoja na marago ya Walawi katikati ya marago yote; kama wapangavyo marago, watasafiri vivyo, kila mtu mahali pake, penye beramu zao.
18 Upande wa magharibi kutakuwa na beramu ya marago ya Efraimu kwa majeshi yao; na mkuu wa wana wa Efraimu atakuwa Elishama mwana wa Amihudi.
19 Na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao walikuwa arobaini elfu na mia tano.
20 Na karibu naye itakuwa kabila ya Manase; na mkuu wa wana wa Manase atakuwa Gamalieli mwana wa Pedasuri;
21 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa thelathini na mbili elfu na mia mbili;
22 tena kabila ya Benyamini; na mkuu wa wana wa Benyamini atakuwa Abidani mwana wa Gideoni;
23 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa thelathini na tano elfu na mia nne.
24 Wote waliohesabiwa katika marago ya Efraimu walikuwa mia na nane elfu na mia moja, kwa majeshi yao. Nao ndio watakaosafiri katika mahali pa tatu.
25 Upande wa kaskazini kutakuwa na beramu ya marago ya Dani kwa majeshi yao; na mkuu wa wana wa Dani atakuwa Ahiezeri mwana wa Amishadai.
26 Na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa sitini na mbili elfu na mia saba.
27 Na hao watakaopanga karibu naye ni kabila ya Asheri; na mkuu wa wana wa Asheri atakuwa Pagieli mwana wa Okrani;
28 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa arobaini na moja elfu na mia tano;
29 kisha kabila ya Naftali; na mkuu wa wana wa Naftali atakuwa Ahira mwana wa Enani;
30 na jeshi lake, na wale waliohesabiwa kwao, walikuwa hamsini na tatu elfu na mia nne.
31 Wote waliohesabiwa katika marago ya Dani walikuwa mia na hamsini na saba elfu na mia sita. Hao ndio watakaosafiri mwisho kwa kuandama beramu zao.
32 Hao ndio waliohesabiwa katika wana wa Israeli kwa nyumba za baba zao; wote waliohesabiwa katika marago kwa majeshi yao, walikuwa mia sita na tatu elfu na mia tano na hamsini.
33 Lakini Walawi hawakuhesabiwa katika wana wa Israeli; kama Bwana alivyomwagiza Musa.
34 Ndivyo walivyofanya wana wa Israeli; kama yote Bwana aliyomwagiza Musa, ndivyo walivyopanga penye beramu zao, na ndivyo walivyosafiri, kila mtu kwa jamaa zao, kwa nyumba za baba zao.