0:00
0:00

Mlango 12

Katika mwaka wa saba wa Yehu, Yoashi alianza kutawala; akatawala miaka arobaini huko Yerusalemu; na jina la mama yake aliitwa Sibia wa Beer-sheba.
2 Yoashi akafanya yaliyo mema machoni pa Bwana siku zake zote Yehoyada kuhani alizomfundisha.
3 Ila mahali pa juu hapakuondolewa; watu wakaendelea kutoa sadaka na kufukiza uvumba katika mahali pa juu.
4 Yoashi akawaambia makuhani, Fedha yote ya vitu vitakatifu iliyoletwa nyumbani mwa Bwana, fedha ya matumizi, fedha ya watu kadiri alivyoandikiwa kila mtu, na fedha yote iliyoletwa kama mtu ye yote aonavyo moyoni mwake kuileta nyumbani mwa Bwana,
5 makuhani na waitwae, kila mtu kwa hao awajuao; nao watatengeneza palipobomoka nyumbani, kila mahali palipoonekana pamebomoka.
6 Lakini ikawa, mwaka wa ishirini na tatu wa mfalme Yoashi, makuhani walikuwa hawajatengeneza mabomoko ya nyumba.
7 Ndipo mfalme Yoashi akamwita Yehoyada kuhani, na makuhani wengine, akawauliza, Mbona hamtengenezi mabomoko ya nyumba? Basi sasa msipokee tena fedha kwa hao mwajuao, lakini itoeni kwa ajili ya mabomoko ya nyumba.
8 Nao makuhani wakakubali kwamba wasipokee fedha kwa watu, wala wasitengeneze mabomoko ya nyumba.
9 Lakini Yehoyada kuhani akatwaa kasha, akatoboa tundu katika kifuniko chake, akaliweka karibu na madhabahu, upande wa kuume mtu aingiapo nyumbani mwa Bwana; na makuhani, waliolinda mlangoni, wakatia ndani yake fedha yote iliyoletwa nyumbani mwa Bwana.
10 Ikawa, walipoona ya kuwa fedha nyingi imo kashani, karani wa mfalme akapanda na kuhani mkuu, wakaifunga mifukoni, wakaihesabu fedha iliyoonekana nyumbani mwa Bwana.
11 Na fedha iliyopimwa wakawapa mikononi wale waliofanya kazi, walioisimamia nyumba ya Bwana; na hao wakawatolea maseremala na wajenzi walioifanya kazi katika nyumba ya Bwana,
12 na hao waashi, na wakata mawe, tena kununua miti na mawe ya kuchongwa, ili kuyatengeneza mabomoko ya nyumba ya Bwana, tena kwa gharama zote za kuitengeneza nyumba.
13 Lakini havikufanywa kwa nyumba ya Bwana vikombe vya fedha, wala makasi, wala mabakuli, wala panda, wala vyombo vyo vyote vya dhahabu, wala vyombo vya fedha, kwa hiyo fedha iliyoletwa nyumbani mwa Bwana;
14 kwa sababu hiyo fedha waliwapa watenda kazi, wakaitengeneza kwayo nyumba ya Bwana.
15 Walakini hawakufanya hesabu na hao watu, waliokabidhiwa fedha hiyo ili wawape watenda kazi; kwa kuwa walitenda kwa uaminifu.
16 Lakini fedha ya matoleo ya kosa, na fedha ya matoleo ya dhambi, haikuletwa nyumbani mwa Bwana; hiyo ilikuwa ya makuhani wenyewe.
17 Ndipo akakwea Hazaeli mfalme wa Shamu akapigana na Gathi, akautwaa; Hazaeli akaelekeza uso ili akwee kwenda Yerusalemu.
18 Yoashi mfalme wa Yuda akavitwaa vyote alivyoviweka wakfu Yehoshafati, na Yehoramu, na Ahazia, baba zake, wafalme wa Yuda, navyo vyote alivyoweka wakfu mwenyewe, na dhahabu yote iliyoonekana katika hazina za nyumba ya Bwana, na nyumba ya mfalme, akamletea Hazaeli mfalme wa Shamu; basi akaenda zake kutoka Yerusalemu.
19 Basi mambo yote ya Yoashi yaliyosalia, na yote aliyoyafanya, je! Hayakuandikwa katika kitabu-cha-tarehe cha wafalme wa Yuda?
20 Nao watumishi wake wakaondoka, wakafanya fitina, wakamwua Yoashi katika nyumba ya Milo, hapo panaposhukia Sila.
21 Kwa maana Yozakari mwana wa Shimeathi, na Yehozabadi mwana wa Shomeri, watumishi wake, wakampiga, naye akafa; wakamzika pamoja na babaze mjini mwa Daudi. Na Amazia mwanawe akatawala mahali pake.