0:00
0:00

Mlango 10

Mainzi mafu huvundisha marhamu ya mwuza marashi; Kadhalika upumbavu haba ni mzito kuliko hekima na heshima.
2 Moyo wake mwenye hekima upo upande wa kuume; Bali moyo wake mpumbavu upo mkono wa kushoto.
3 Naam, huyo mpumbavu tena, aendapo njiani, hupungukiwa na fahamu zake; hata humwambia kila mtu ya kuwa yeye ni mpumbavu.
4 Roho yake mtawala ikiinuka kinyume chako, Usiondoke mara mahali pako ulipo; Kwa maana roho ya upole hutuliza machukizo yaliyo makubwa.
5 Liko baa nililoliona chini ya jua, nalo ni kama kosa litokalo kwake yeye atawalaye;
6 ya kuwa upumbavu huwekwa mahali pa juu sana, nao wakwasi hukaa mahali pa chini.
7 Mimi nimeona watumwa wamepanda farasi, na wakuu wakienda kwa miguu juu ya nchi kama watumwa.
8 Mwenye kuchimba shimo atatumbukia ndani yake; Na yeye abomoaye boma, nyoka atamwuma.
9 Mwenye kuchonga mawe ataumizwa kwayo; Naye apasuaye miti huona hatari katika hiyo.
10 Iwapo chuma hakipati, wala mtu hakinoi; Ndipo hana budi kutumia nguvu zaidi. Walakini yafaa kutumia hekima, na kufanikiwa.
11 Nyoka akiuma asijatumbuizwa, Basi hakuna faida ya mtumbuizi.
12 Maneno ya kinywa chake mwenye hekima yana neema; Bali midomo ya mpumbavu itammeza nafsi yake.
13 Mwanzo wa maneno ya kinywa chake ni upuuzi; na mwisho wa usemi wake ni wazimu wenye hatari.
14 Tena, upumbavu huongeza maneno; lakini mwanadamu hajui yatakayokuwako; nayo yatakayokuwa baada yake, ni nani awezaye kumweleza?
15 Kazi yao wapumbavu huwachosha kila mmoja, Maana hajui hata njia ya kuuendea mji.
16 Ole wako, nchi, akiwa mfalme wako ni kijana, Na wakuu wako hula asubuhi!
17 Heri kwako, nchi, mfalme wako akiwa mtoto wa watu, Na wakuu wako hula wakati ufaao, Ili makusudi wapate nguvu, wala si kwa ajili ya ulevi.
18 Kwa sababu ya uvivu paa hunepa; Na kwa utepetevu wa mikono nyumba huvuja.
19 Karamu hufanywa kwa ajili ya kicheko, Na divai huyafurahisha maisha; Na fedha huleta jawabu la mambo yote.
20 Usimlaani mfalme, la, hata katika wazo lako; Wala usiwalaani wakwasi chumbani mwako; Kwa kuwa ndege wa anga ataichukua sauti, Na mwenye mabawa ataitoa habari.