Wimbo Ulio Bora

1 2 3 4 5 6 7 8

0:00
0:00

Mlango 8

Laiti ungekuwa kama ndugu yangu, Aliyeyanyonya matiti ya mamangu! Kama ningekukuta huko nje, Ningekubusu, asinidharau mtu.
2 Ningekuongoza nyumbani mwa mamangu, Naye angenifundisha; Ningekunywesha divai iliyokolea,Divai mpya ya mkomamanga wangu.
3 Mkono wake wa kushoto ungekuwa chini ya kichwa changu, Nao wa kuume ungenikumbatia.
4 Nawasihi, enyi binti za Yerusalemu, Kwani kuyachochea mapenzi, au kuyaamsha, Hata yatakapoona vema?
5 Ni nani huyu apandaye kutoka nyikani, Akimtegemea mpendwa wake? Nalikuamsha chini ya huo mpera; Huko mama yako alikuonea utungu, Aliona utungu aliyekuzaa.
6 Nitie kama muhuri moyoni mwako, Kama muhuri juu ya mkono wako; Kwa maana upendo una nguvu kama mauti, Na wivu ni mkali kama ahera. Mwako wake ni mwako wa moto, Na miali yake ni miali ya Yahu.
7 Maji mengi hayawezi kuuzimisha upendo, Wala mito haiwezi kuuzamisha; Kama mtu angetoa badala ya upendo Mali yote ya nyumbani mwake, Angedharauliwa kabisa.
8 Kwetu sisi tuna umbu mdogo, Wala hana maziwa; Tumfanyieje umbu letu, Siku atakapoposwa?
9 Kama akiwa tu ukuta, Tumjengee buruji za fedha; Na kama akiwa ni mlango, Tumhifadhi kwa mbao za mierezi.
10 Mimi nalikuwa ukuta, Na maziwa yangu kama minara; Ndipo nikawa machoni pake Kama mtu aliyeipata amani.
11 Sulemani alikuwa na shamba la mizabibu huko Baal-hamomi Akawakodisha walinzi hilo shamba lake la mizabibu; Kila mtu atoe vipande elfu vya fedha kwa matunda yake.
12 Shamba langu la mizabibu, lililo langu mimi, li mbele yangu. Basi, Sulemani, wewe uwe na elfu zako, Na hao wayalindao matunda yake wapewe mia mbili.
13 Wewe ukaaye bustanini, Hao rafiki huisikiliza sauti yako; Unisikizishe mimi.
14 Ukimbie, mpendwa wangu, Nawe uwe kama paa, au ayala, Juu ya milima ya manukato.