0:00
0:00

Mlango 18

Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, kusema,
2 Ondoka, ukashuke mpaka nyumba ya mfinyanzi, na huko nitakusikizisha maneno yangu.
3 Basi nikashuka mpaka nyumba ya mfinyanzi, na tazama, alikuwa akifanya kazi yake kwa magurudumu.
4 Na chombo kile, alichokuwa akikifinyanga, kilipoharibika mkononi mwake yule mfinyanzi, alikifanyiza tena kuwa chombo kingine, kama alivyoona vema yule mfinyanzi kukifanya.
5 Ndipo neno la Bwana likanijia, kusema,
6 Ee nyumba ya Israeli, je! Siwezi mimi kuwatendea ninyi vile vile kama mfinyanzi huyu alivyotenda? Asema Bwana. Angalieni, kama udongo ulivyo katika mkono wa mfinyanzi, ndivyo mlivyo ninyi katika mkono wangu, Ee nyumba ya Israeli.
7 Wakati wo wote nitakapotoa habari za taifa, na habari za ufalme, kuung'oa, na kuuvunja, na kuuangamiza;
8 ikiwa taifa lile nililolitaja litageuka, na kuacha maovu yake nitaghairi, nisitende mabaya yale niliyoazimia kuwatenda.
9 Na wakati wo wote nitakapotoa habari za taifa, na habari za ufalme, kuujenga na kuupanda,
10 ikiwa watatenda maovu mbele za macho yangu, wasiitii sauti yangu, basi nitaghairi, nisitende mema yale niliyoazimia kuwatendea.
11 Haya! Basi, ukawaambie watu wa Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu, ukisema, Bwana asema hivi, Tazama, ninafinyanga mabaya juu yenu, na kuwaza mawazo juu yenu; rudini sasa, kila mmoja na aiache njia yake mbaya; zitengenezeni njia zenu, na matendo yenu.
12 Lakini wao wasema, Hapana tumaini lo lote; maana sisi tutafuata mawazo yetu wenyewe, nasi tutatenda kila mmoja wetu kwa kuufuata ushupavu wa moyo wake mbaya.
13 Basi, kwa ajili ya hayo, Bwana asema hivi, Ulizeni sasa katika mataifa, ni nani aliyesikia habari za mambo kama hayo; bikira wa Israeli ametenda tendo lichukizalo sana.
14 Je! Theluji ya Lebanoni itakoma katika jabali la kondeni? Au je! Maji ya baridi yashukayo toka mbali yatakauka?
15 Maana watu wangu wamenisahau, wameufukizia ubatili uvumba; nao wamewakaza katika njia zao, katika mapito ya zamani, ili wapite katika njia za kando, katika njia isiyotengenezwa;
16 ili kufanya nchi yao kuwa kitu cha kushangaza, na cha kuzomewa daima; kila mtu apitaye karibu nayo atashangaa, na kutikisa kichwa chake.
17 Nami nitawatawanya mbele ya adui, kama kwa upepo wa mashariki; nami nitaviangalia visogo vyao, wala si nyuso zao, siku ya msiba wao.
18 Hapo ndipo waliposema, Njoni na tufanye mashauri juu ya Yeremia; maana sheria haitampotea kuhani, wala shauri halitampotea mwenye hekima, wala neno halitampotea nabii. Njoni, na tumpige kwa ndimi zetu, wala tusiyaangalie maneno yake yo yote.
19 Niangalie, Ee Bwana, ukasikilize sauti ya wanaoshindana nami.
20 Je! Mabaya yalipwe badala ya mema? Maana wameichimbia nafsi yangu shimo. Kumbuka jinsi nilivyosimama mbele zako, ili niseme mema kwa ajili yao, nikaigeuze ghadhabu yako isiwapate.
21 Kwa sababu hiyo, uwatoe watoto wao waone njaa, uwatoe nguvu za upanga ziwapate; wake zao wafiwe na watoto wao, na kufiwa na waume zao; wanaume wao wauawe, na vijana wao wapigwe kwa upanga vitani.
22 Kilio na kisikiwe kitokacho katika nyumba zao, hapo utakapoleta kikosi juu yao kwa ghafula; kwa maana wamenichimbia shimo waninase, nao wameifichia miguu yangu mitego.
23 Lakini wewe, Bwana, unajua mashauri yao yote juu yangu, ya kuniua; usiwasamehe uovu wao, wala usifute dhambi yao mbele za macho yako; bali wakwazwe mbele zako; uwatende mambo wakati wa hasira yako.