0:00
0:00

Mlango 13

Hii ndiyo mara ya tatu ya mimi kuja kwenu. Kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno litathibitishwa.
2 Nimetangulia kuwaambia; na, kama vile nilipokuwapo mara ya pili, vivyo hivyo sasa nisipokuwapo, nawaambia wazi wao waliotenda dhambi tangu hapo, na wengine wote, ya kwamba, nikija, sitahurumia;
3 kwa kuwa mnatafuta dalili ya Kristo, asemaye ndani yangu, ambaye si dhaifu kwenu, bali ana uweza ndani yenu.
4 Maana, alisulibiwa katika udhaifu, lakini anaishi kwa nguvu za Mungu. Maana sisi nasi tu dhaifu katika yeye; lakini tutaishi pamoja naye kwa uweza wa Mungu ulio kwenu.
5 Jijaribuni wenyewe kwamba mmekuwa katika imani; jithibitisheni wenyewe. Au hamjijui wenyewe, kwamba Yesu Kristo yu ndani yenu? Isipokuwa mmekataliwa.
6 Lakini natumaini kama mtajua ya kuwa sisi hatukukataliwa.
7 Nasi twamwomba Mungu, msifanye lo lote lililo baya; si kwamba sisi tuonekane tumekubaliwa, lakini ninyi mfanye lile lililo jema, tujapokuwa sisi tu kama waliokataliwa.
8 Maana hatuwezi kutenda neno lo lote kinyume cha kweli, bali kwa ajili ya kweli.
9 Maana twafurahi, iwapo sisi tu dhaifu, nanyi mmekuwa hodari. Tena twaomba hili nalo, kutimilika kwenu.
10 Kwa sababu hiyo, naandika haya nisipokuwapo, ili, nikiwapo, nisiutumie ukali kwa kadiri ya uwezo ule niliopewa na Bwana, kwa kujenga wala si kwa kubomoa.
11 Hatimaye, ndugu, kwaherini; mtimilike, mfarijike, nieni mamoja, mkae katika amani; na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi.
12 Salimianeni kwa busu takatifu.
13 Watakatifu wote wawasalimu.
14 Neema ya Bwana Yesu Kristo, na pendo la Mungu, na ushirika wa Roho Mtakatifu ukae nanyi nyote.