0:00
0:00

Mlango 7

Na baada ya hayo Yesu alikuwa akitembea katika Galilaya; maana hakutaka kutembea katika Uyahudi, kwa sababu Wayahudi walikuwa wakitafuta kumwua.
2 Na sikukuu ya Wayahudi, Sikukuu ya Vibanda, ilikuwa karibu.
3 Basi ndugu zake wakamwambia, Ondoka hapa, uende Uyahudi, wanafunzi wako nao wapate kuzitazama kazi zako unazozifanya.
4 Kwa maana hakuna mtu afanyaye neno kwa siri, naye mwenyewe ataka kujulikana. Ukifanya mambo haya, basi jidhihirishe kwa ulimwengu.
5 Maana hata nduguze hawakumwamini.
6 Basi Yesu akawaambia, Haujafika bado wakati wangu; ila wakati wenu sikuzote upo.
7 Ulimwengu hauwezi kuwachukia ninyi; bali hunichukia mimi, kwa sababu mimi naushuhudia ya kuwa kazi zake ni mbovu.
8 Kweeni ninyi kwenda kula sikukuu; mimi sikwei bado kwenda kula sikukuu hii, kwa kuwa haujatimia wakati wangu.
9 Naye alipokwisha kuwaambia hayo, alikaa vivi hivi huko Galilaya.
10 Hata ndugu zake walipokwisha kukwea kuiendea sikukuu, ndipo yeye naye alipokwea, si kwa wazi bali kana kwamba kwa siri.
11 Basi Wayahudi wakamtafuta kwenye sikukuu, wakasema, Yuko wapi yule?
12 Kukawa na manung'uniko mengi katika makutano juu yake. Wengine wakasema, Ni mtu mwema. Na wengine wakasema, Sivyo; bali anawadanganya makutano.
13 Walakini hakuna mtu aliyemtaja waziwazi, kwa sababu ya kuwaogopa Wayahudi.
14 Hata ikawa katikati ya sikukuu Yesu alikwea kuingia hekaluni, akafundisha.
15 Wayahudi wakastaajabu wakisema, Amepataje huyu kujua elimu, ambaye hakusoma?
16 Basi Yesu akawajibu, akasema, Mafunzo yangu si yangu mimi, ila ni yake yeye aliyenipeleka.
17 Mtu akipenda kuyatenda mapenzi yake, atajua habari ya yale mafunzo, kwamba yatoka kwa Mungu, au kwamba mimi nanena kwa nafsi yangu tu.
18 Yeye anenaye kwa nafsi yake tu hutafuta utukufu wake mwenyewe; bali yeye anayetafuta utukufu wake aliyempeleka, huyo ni wa kweli, wala ndani yake hamna udhalimu.
19 Je! Musa hakuwapa torati? Wala hakuna mmoja wenu aitendaye torati. Mbona mnatafuta kuniua?
20 Mkutano wakajibu, Ama! Una pepo! Ni nani anayetafuta kukuua?
21 Yesu akajibu, akawaambia, Mimi nalitenda kazi moja, nanyi nyote mnaistaajabia.
22 Musa aliwapa tohara; lakini si kwamba yatoka kwa Musa, bali kwa mababa; nanyi siku ya sabato humtahiri mtu.
23 Basi ikiwa mtu hupashwa tohara siku ya sabato, ili torati ya Musa isije ikavunjika, mbona mnanikasirikia mimi kwa sababu nalimfanya mtu kuwa mzima kabisa siku ya sabato?
24 Basi msihukumu hukumu ya macho tu, bali ifanyeni hukumu iliyo ya haki.
25 Basi baadhi ya watu wa Yerusalemu wakasema, Je! Huyu siye wanayemtafuta ili wamwue?
26 Na kumbe! Anena waziwazi, wala hawamwambii neno! Yamkini hao wakuu wanajua hakika ya kuwa huyu ndiye Kristo?
27 Lakini huyu twamjua atokako; bali Kristo atakapokuja hakuna ajuaye atokako.
28 Basi Yesu akapaza sauti yake hekaluni, akifundisha na kusema, Mimi mnanijua, na huko nitokako mnakujua; wala sikuja kwa nafsi yangu; ila yeye aliyenipeleka ni wa kweli, msiyemjua ninyi.
29 Mimi namjua, kwa kuwa nimetoka kwake, naye ndiye aliyenituma.
30 Basi wakatafuta kumkamata; lakini hakuna mtu aliyeunyosha mkono wake ili kumshika, kwa sababu saa yake ilikuwa haijaja bado.
31 Na watu wengi katika mkutano wakamwamini; wakasema, Atakapokuja Kristo, je! Atafanya ishara nyingi zaidi kuliko hizi alizozifanya huyu?
32 Mafarisayo wakawasikia mkutano wakinung'unika hivi juu yake; basi wakuu wa makuhani na Mafarisayo wakatuma watumishi ili wamkamate.
33 Basi Yesu akasema, Bado kitambo kidogo nipo pamoja nanyi; kisha naenda zangu kwake yeye aliyenipeleka.
34 Mtanitafuta wala hamtaniona; nami nilipo ninyi hamwezi kuja.
35 Basi Wayahudi wakasemezana, Huyu atakwenda wapi hata sisi tusimwone? Ati! Atakwenda kwa Utawanyiko wa Wayunani, na kuwafundisha Wayunani?
36 Ni neno gani hilo alilolisema, Mtanitafuta wala hamtaniona; nami nilipo ninyi hamwezi kuja?
37 Hata siku ya mwisho, siku ile kubwa ya sikukuu, Yesu akasimama, akapaza sauti yake akisema, Mtu akiona kiu, na aje kwangu anywe.
38 Aniaminiye mimi, kama vile maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake.
39 Na neno hilo alilisema katika habari ya Roho, ambaye wale wamwaminio watampokea baadaye; kwa maana Roho alikuwa hajaja, kwa sababu Yesu alikuwa hajatukuzwa.
40 Basi wengine katika mkutano walipoyasikia maneno hayo, walisema, Hakika huyu ndiye nabii yule.
41 Wengine walisema, Huyu ndiye Kristo. Wengine wakasema, Je! Kristo atoka Galilaya?
42 Andiko halikusema ya kwamba Kristo atoka katika uzao wa Daudi, na kutoka Bethlehemu, mji ule alioukaa Daudi?
43 Basi kukaingia matengano katika mkutano kwa ajili yake.
44 Baadhi yao wakataka kumkamata, lakini hakuna mtu aliyenyosha mikono yake ili kumshika.
45 Basi wale watumishi wakawaendea wakuu wa makuhani na Mafarisayo. Nao wakawaambia, Mbona hamkumleta?
46 Wale watumishi wakajibu. Hajanena kamwe mtu ye yote kama huyu anavyonena.
47 Basi Mafarisayo wakawajibu, Je! Ninyi nanyi mmedanganyika?
48 Ni nani katika wakuu amwaminiye, au katika Mafarisayo?
49 Lakini makutano hawa wasioifahamu torati wamelaaniwa.
50 Akawaambia Nikodemo, (naye ni yule aliyemwendea zamani, maana ni mmoja wao),
51 Je! Torati yetu humhukumu mtu kabla ya kumsikia kwanza, na kujua atendavyo?
52 Wakajibu, wakamwambia, Je! Wewe nawe umetoka Galilaya!
53 Tafuta, ukaone ya kuwa kutoka Galilaya hakutokea nabii.