Uwezo na nguvu

0:00
0:00

  • kwa maana Bwana, Mungu wenu, ndiye awaandamaye kwenda kuwapigania juu ya adui zenu, ili kuwaokoa ninyi.
    Kumbukumbu la Torati 20:4
  • Kisha Daudi akamwambia Sulemani mwanawe, Uwe hodari, mwenye moyo mkuu, ukatende hivyo; usiogope wala usifadhaike; kwa kuwa Bwana, Mungu, Mungu wangu, yu pamoja nawe; yeye hatakupungukia wala kukuacha, hata itakapomalizika kazi yote ya huo utumishi wa nyumba ya Bwana.
    1 Mambo ya Nyakati 28:20
  • kwake upo mkono wa mwili; ila kwetu yupo Bwana, Mungu wetu, kutusaidia, na kutupigania mapigano yetu. Na watu wakayategemea maneno ya Hezekia, mfalme wa Yuda.
    2 Mambo ya Nyakati 32:8
  • Vinywani mwa watoto wachanga na wanyonyao Umeiweka misingi ya nguvu; Kwa sababu yao wanaoshindana nawe; Uwakomeshe adui na mijilipiza kisasi.
    Zaburi 8:2
  • Maana kwa msaada wako nafuatia jeshi, Kwa msaada wa Mungu wangu naruka ukuta. Mungu, njia yake ni kamilifu, Ahadi ya Bwana imehakikishwa, Yeye ndiye ngao yao. Wote wanaomkimbilia. Mungu ndiye anifungaye mshipi wa nguvu, Naye anaifanya kamilifu njia yangu.
    Zaburi 18:29, 30, 32
  • Hawa wanataja magari na hawa farasi, Bali sisi tutalitaja jina la Bwana, Mungu wetu.
    Zaburi 20:7
  • Naamini ya kuwa nitauona wema wa Bwana Katika nchi ya walio hai. Umngoje Bwana, uwe hodari, Upige moyo konde, naam, umngoje Bwana.
    Zaburi 27:13, 14
  • Bwana ni nguvu zangu na ngao yangu. Moyo wangu umemtumaini, Nami nimesaidiwa; Basi, moyo wangu unashangilia, Na kwa wimbo wangu nitamshukuru. Bwana ni nguvu za watu wake, Naye ni ngome ya wokovu kwa masihi wake.
    Zaburi 28:7, 8
  • Na wokovu wa wenye haki una Bwana; Yeye ni ngome yao wakati wa taabu.
    Zaburi 37:39
  • Mwili wangu na moyo wangu hupunguka, Bali Mungu ni mwamba wa moyo wangu Na sehemu yangu milele.
    Zaburi 73:26
  • Heri ambaye nguvu zake zatoka kwako, Na njia ziendazo Sayuni zimo moyoni mwake. Huendelea toka nguvu hata nguvu, Huonekana Sayuni kila mmoja mbele za Mungu.
    Zaburi 84:5, 7
  • Bwana ni nguvu zangu na wimbo wangu, Naye amekuwa wokovu wangu.
    Zaburi 118:14
  • Nafsi yangu imeyeyuka kwa uzito, Unitie nguvu sawasawa na neno lako.
    Zaburi 119:28
  • Maana umekuwa ngome ya maskini, Ngome ya mhitaji katika dhiki yake, Mahali pa kukimbilia wakati wa tufani, Kivuli wakati wa hari; Wakati uvumapo upepo wa watu watishao, Kama dhoruba ipigayo ukuta.
    Isaya 25:4
  • Huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo.
    Isaya 40:29
  • usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu.
    Isaya 41:10
  • Yesu akawakazia macho, akawaambia, Kwa wanadamu hilo haliwezekani; bali kwa Mungu yote yawezekana.
    Mathayo 19:26
  • Basi, tuseme nini juu ya hayo? Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu?
    Warumi 8:31
  • Si kwamba twatosha sisi wenyewe kufikiri neno lo lote kwamba ni letu wenyewe, bali utoshelevu wetu watoka kwa Mungu.
    2 Wakorintho 3:5
  • (maana silaha za vita vyetu si za mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome;)
    2 Wakorintho 10:4
  • Naye akaniambia, Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu. Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa Kristo ukae juu yangu. Kwa hiyo napendezwa na udhaifu, na ufidhuli, na misiba, na adha, na shida, kwa ajili ya Kristo. Maana niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu.
    2 Wakorintho 12:9, 10
  • awajalieni, kwa kadiri ya utajiri wa utukufu wake, kufanywa imara kwa nguvu, kwa kazi ya Roho wake katika utu wa ndani.
    Waefeso 3:16
  • Hatimaye, mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake.
    Waefeso 6:10
  • Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.
    Wafilipi 4:13
  • Toka mwisho wa nchi nitakulilia nikizimia moyo, Uniongoze juu ya mwamba nisioweza kuupanda.
    Zaburi 61:2
  • Kwa maana atamkomboa mhitaji aliapo, Na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi.
    Zaburi 72:12
  • Siku ile niliyokuita uliniitikia, Ukanifariji nafsi kwa kunitia nguvu.
    Zaburi 138:3
  • bali wao wamngojeao Bwana watapata nguvu mpya; watapanda juu kwa mbawa kama tai; watapiga mbio, wala hawatachoka; watakwenda kwa miguu, wala hawatazimia.
    Isaya 40:31
  • Je! Si mimi niliyekuamuru? Uwe hodari na moyo wa ushujaa; usiogope wala usifadhaike; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, yu pamoja nawe kila uendako.
    Yoshua 1:9
  • Kwa sababu hiyo Bwana, Mungu wa majeshi, asema hivi, Kwa sababu mnasema neno hili, tazama, nitafanya maneno yangu katika kinywa chako kuwa moto, na watu hawa kuwa kuni, nao moto utawala.
    Yeremia 5:14
  • Nami nitawatia nguvu katika Bwana; nao watatembea huko na huko katika jina lake, asema Bwana.
    Zekaria 10:12
  • Kwa kuwa si ninyi msemao, bali ni Roho wa Baba yenu asemaye ndani yenu.
    Mathayo 10:20
  • Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.
    Matendo ya Mitume 1:8
  • Basi walipoona ujasiri wa Petro na Yohana, na kuwajua ya kuwa ni watu wasio na elimu, wasio na maarifa, wakastaajabu, wakawatambua ya kwamba walikuwa pamoja na Yesu.
    Matendo ya Mitume 4:13
  • Kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu.
    1 Wakorintho 1:18
  • Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu.
    1 Wakorintho 2:4, 5