0:00
0:00

Mlango 19

Bwana, Mungu wako, atakapoyakatilia mbali hayo mataifa yenye nchi akupayo Bwana, Mungu wako, nawe ukawafuata, na kukaa katika miji yao, na katika nyumba zao;
2 itenge miji mitatu iwe kwako katikati ya nchi yako, akupayo Bwana, Mungu wako, kuimiliki.
3 Itengeze njia, igawanye na mipaka ya nchi yako, akurithishayo Bwana, Mungu wako, iwe mafungu matatu, ili kwamba kila mwenye kuua mtu apate kukimbilia huko.
4 Na hii ndiyo hukumu ya mwenye kuua mtu, atakayekimbilia huko awe hai; atakayemwua mwenziwe pasipo kukusudia, wala hakumchukia tangu hapo;
5 kama aingiapo mtu na mwenziwe mwituni kwenda kukata kuni, akapeleka mkono wake na shoka ili kukata mti, likatoka shoka katika mpini, likampiga yule mwenziwe hata akafa; basi na akimbilie katika miji hii mmojawapo awe hai;
6 asije akaandamiwa mwuaji na mwenye kulipiza kisasi cha damu, moyo wake ukali na hasira, akampata kwa njia kuwa ndefu, akamwua; wala hana haki ya kuuawa, kwa kuwa hakumchukia tangu hapo.
7 Kwa sababu hii ninakuamuru, na kukuambia, Ujitengee miji mitatu.
8 Na kama Bwana, Mungu wako, akiueneza mpaka wako kama alivyowaapia baba zako, akakupa na nchi yote aliyoahidi kwamba atawapa baba zako;
9 nawe ukiyashika maagizo haya yote nikuagizayo leo, na kuyafanya, kumpenda Bwana, Mungu wako, na kwenda sikuzote katika njia zake, ndipo ujiongezee miji mitatu tena, pamoja na mitatu ile;
10 isije ikamwagika damu ya asiye makosa kati ya nchi yako akupayo Bwana, Mungu wako, iwe urithi, ikawa na damu juu yako.
11 Lakini mtu awaye yote akimchukia mwenziwe na kumwotea na kumwinukia, akampiga hata akafa; naye akakimbilia miji hii mmojawapo;
12 ndipo wazee wa mji wake wapeleke ujumbe kumtwaa huko, na kumuua katika mkono wa mwenye kulipiza kisasi cha damu, apate kufa.
13 Jicho lako lisimhurumie, lakini uondoe damu ya asiye makosa katika Israeli, ili upate kufanikiwa.
14 Usiiondoe alama ya mpaka wa jirani yako, waliouweka watu wa kale katika urithi wako, utakaorithi ndani ya nchi akupayo Bwana, Mungu wako, uimiliki.
15 Shahidi mmoja asimwinukie mtu awaye yote kumshuhudia kwa uovu wo wote, wala kwa dhambi yo yote, katika makosa akosayo yo yote; jambo na lithibitishwe kwa vinywa vya mashahidi wawili, au watatu.
16 Shahidi mdhalimu akimwinukia mtu ye yote na kushuhudia juu yake ya upotoe;
17 ndipo wale watu washindanao kwa mambo yale na wasimame wote wawili mbele za Bwana, mbele ya makuhani na waamuzi watakaokuwapo siku hizo;
18 nao waamuzi na watafute kwa bidii; na tazama, yule shahidi akiwa shahidi wa uongo, naye ametoa ushahidi wa uongo juu ya nduguye;
19 ndipo mtamfanyia kama alivyodhani kumfanyia nduguye; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati yako.
20 Na watakaosalia watasikia na kuogopa, wasifanye tena uovu mfano wa huo katikati yako.
21 Wala jicho lako lisiwe na huruma; uzima kwa uzima, jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono, mguu kwa mguu.