0:00
0:00

Mlango 2

Ndipo tukageuka, tukashika safari yetu kwenda jangwani kwa njia ya Bahari ya Shamu, kama alivyoniambia Bwana; tukawa kuizunguka milima ya Seiri siku nyingi.
2 Bwana akanena, akaniambia,
3 Mlivyouzunguka mlima huu vyatosha; geukeni upande wa kaskazini.
4 Nawe waagize watu, uwaambie, Mtapita kati ya mpaka wa ndugu zenu wana wa watu, uwaambie, Mtapita kati ya mpaka wa ndugu zenu wana wa Esau waketio Seiri; nao watawaogopa; basi jiangalieni nafsi zenu sana;
5 msitete nao; kwa maana sitawapa katika nchi yao kamwe, hata kiasi cha kukanyaga wayo wa mguu; kwa kuwa nimempa Esau milima ya Seiri kuwa milki yake.
6 Nunueni vyakula kwao kwa fedha, mpate kula; na maji nayo nunueni kwao kwa fedha, mpate kunywa.
7 Kwa kuwa Bwana, Mungu wako, amekubarikia katika kazi yote ya mkono wako; amejua ulivyotembea katika jangwa kubwa hili; miaka arobaini hii alikuwa nawe Bwana, Mungu wako; hukukosa kitu.
8 Basi tukapita kando yao ndugu zetu wana wa Esau, waketio Seiri kutoka njia ya Araba, kutoka Elathi na kutoka Esion-geberi. Tukageuka tukapita njia ya bara ya Moabu.
9 Bwana akaniambia, usiwasumbue Wamoabi, wala usishindane nao katika mapigano; kwa kuwa sitakupa katika nchi yake kuimiliki; kwa sababu Ari nimewapa wana wa Lutu kuimiliki.
10 (Walioketi humo hapo kale ni Waemi, nao ni watu wakubwa, wengi, warefu, mfano wa Waanaki;
11 na hawa nao wadhaniwa kuwa majitu kama Waanaki;lakini Wamoabi huwaita Waemi.
12 Na Wahori nao walikuwa wakikaa Seiri hapo kale, lakini wana wa Esau waliwafuata; wakawaangamiza mbele yao, wakakaa badala yao; kama alivyofanya Israeli nchi ya milki yake aliyopewa na Bwana.)
13 Sasa basi ondokeni, mkakivuke kijito cha Zeredi. Nasi tukakivuka kile kijito cha Zeredi.
14 Na siku tulizokuwa tukienda kutoka Kadesh-barnea hata tulipovuka kijito cha Zeredi, zilikuwa ni miaka thelathini na minane; maana, hata walipokwisha kuangamizwa watu wa vita kutoka kati ya marago, kizazi chao chote, kama walivyoapiwa na Bwana.
15 Tena mkono wa Bwana ulikuwa juu yao ili kuwaangamiza, kuwatoa kati ya marago, hata walipokoma.
16 Basi ikawa, walipokwisha angamizwa kwa kufa watu wote wa vita kati ya watu,
17 Bwana aliniambia, akasema,
18 Hivi leo ivuke Ari, mpaka wa Moabu;
19 na utakaposongea kuwaelekea wana wa Amoni, usiwasumbue wana wa Amoni, wala usishindane nao; kwa kuwa sitakupa katika nchi ya hao wana wa Amoni kuwa milki yako; kwa sababu nimewapa wana wa Lutu iwe milki yao.
20 (Nchi hiyo nayo yadhaniwa kuwa ni nchi ya Warefai, hapo kale Warefai walikaa humo; lakini Waamoni huwaita Wazamzumi;
21 nao ni watu wengi, wakubwa, warefu, kama Waanaki; lakini Bwana aliwaangamiza mbele yao; wakawafuata wakakaa badala yao;
22 kama vile alivyowafanyia wana wa Esau, waliokaa Seiri, alipowaangamiza Wahori mbele yao; wakawafuata, wakakaa badala yao hata hivi leo;
23 na Waavi waliokuwa wakikaa katika vijiji mpaka Gaza waliangamizwa na Wakaftori waliotoka Kaftori, na hawa wakakaa badala yao.)
24 Ondokeni, mshike safari yenu, mvuke bonde la Arnoni; tazama, nimemtia Sihoni Mwamori mfalme wa Heshboni mkononi mwako, na nchi yake; anzeni kuimiliki, mshindane naye katika mapigano.
25 Hivi leo nitaanza mimi kutia utisho wako na kuhofiwa kwako juu ya watu walio chini ya mbingu kila mahali, watakaosikia uvumi wako, na kutetemeka, na kuingiwa na uchungu kwa sababu yako.
26 Nikatuma wajumbe kutoka bara ya Kedemothi kwenda kwa Sihoni mfalme wa Heshboni na maneno ya amani, kusema.
27 Nipishe katikati ya nchi yako; nitakwenda kwa njia ya barabara, sitageuka kwenda mkono wa kuume wala wa kushoto.
28 Nawe uniuzie chakula kwa fedha nile; unipe na maji kwa fedha, ninywe; ila unipishe katikati kwa miguu yangu, hayo tu;
29 kama walivyonifanyia hao wana wa Esau waketio Seiri, na hao Wamoabi waketio Ari; hata nivuke Yordani niingie nchi tupewayo na Bwana, Mungu wetu.
30 Lakini Sihoni mfalme wa Heshboni hakutuacha kupitia kwake; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, alimfanya mgumu roho yake, akamtia ukaidi moyoni mwake, apate mtia mkononi mwako kama alivyo hivi leo.
31 Kisha Bwana akaniambia, Tazama, nimeanza kumtoa Sihoni na nchi yake mbele yako; anza kuimiliki, upate kuirithi nchi yake.
32 Ndipo Sihoni alipotutokea juu yetu yeye na watu wake wote, kupigana huko Yahasa.
33 Bwana, Mungu wetu, akamtoa mbele yetu, tukampiga yeye na wanawe, na watu wake wote.
34 Tukatwaa miji yake yote wakati huo, tukaharibu kabisa kila mji uliokuwa na watu, pamoja na wanawake na wadogo; tusimsaze hata mmoja;
35 ila ng'ombe zao tuliwatwaa kuwa mawindo yetu, pamoja na nyara za miji tuliyoitwaa.
36 Kutoka Aroeri iliyo katika ukingo wa bonde la Arnoni, na huo mji ulio ndani ya bonde, mpaka kufika Gileadi, hapakuwa na mji uliokuwa mrefu kutushinda; Bwana, Mungu wetu, aliiweka wazi yote mbele yetu; ila nchi ya wana wa Amoni hukuisongelea;
37 upande wote wa mto wa Yaboki, na miji ya nchi ile ya milimani, na kila mahali alipotukataza Bwana, Mungu wetu.