0:00
0:00

Mlango 32

Sikilizeni, enyi mbingu, nami nitanena; Na nchi isikie maneno ya kinywa changu.
2 Mafundisho yangu yatadondoka kama mvua, Maneno yangu yatatona-tona kama umande; Kama manyunyu juu ya majani mabichi; Kama matone ya mvua juu ya mimea.
3 Maana nitalitangaza Jina la Bwana; Mpeni ukuu Mungu wetu.
4 Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; Maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, Yeye ndiye mwenye haki na adili.
5 Wametenda mambo ya uharibifu, Hawawi watoto wake, hii ndiyo ila yao; Wao ni kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka.
6 Je! Mnamlipa Bwana hivi, Enyi watu wapumbavu na ujinga? Je! Yeye siye baba yako aliyekununua? Amekufanya, na kukuweka imara.
7 Kumbuka siku za kale, Tafakari miaka ya vizazi vingi; Mwulize baba yako, naye atakuonyesha; Wazee wako, nao watakuambia.
8 Yeye Aliye Juu alipowapa mataifa urithi wao, Alipowabagua wanadamu, Aliweka mipaka ya watu Kwa kadiri ya hesabu ya wana wa Israeli.
9 Maana, sehemu ya Bwana ni watu wake, Yakobo ni kura ya urithi wake.
10 Alimkuta katika nchi ya ukame, Na katika jangwa tupu litishalo; Alimzunguka, akamtunza; Akamhifadhi kama mboni ya jicho;
11 Mfano wa tai ataharikishaye kioto chake; Na kupapatika juu ya makinda yake, Alikunjua mbawa zake, akawatwaa, Akawachukua juu ya mbawa zake;
12 Bwana peke yake alimwongoza, Wala hapakuwa na mungu mgeni pamoja naye.
13 Alimpandisha mahali pa nchi palipoinuka, Naye akala mazao ya mashamba; Akamnyonyesha asali iliyotoka jabalini, Na mafuta yaliyotoka katika mwamba wa gumegume;
14 Siagi ya ng'ombe, na maziwa ya kondoo, Pamoja na mafuta ya wana-kondoo, Kondoo waume wa Kibashani, na mbuzi, Na unono wa ngano iliyo nzuri; Ukanywa divai, damu ya mizabibu.
15 Lakini Yeshuruni alinenepa, akapiga teke; Umenenepa, umekuwa mnene, umewanda; Ndipo akamwacha Mungu aliyemfanya, Akamdharau Mwamba wa wokovu wake.
16 Wakamtia wivu kwa miungu migeni, Wakamkasirisha kwa machukizo.
17 Walitoa sadaka kwa pepo, si Mungu, Kwa miungu wasiyoijua, Kwa miungu mipya iliyotokea siku zilizo karibu, Ambayo baba zenu hawakuiogopa.
18 Humkumbuki Mwamba aliyekuzaa, Mungu aliyekuzaa umemsahau.
19 Bwana akaona, akawachukia, Kwa sababu ya kukasirishwa na wanawe na binti zake.
20 Akasema, Nitawaficha uso wangu, Nitaona mwisho wao utakuwaje; Maana, ni kizazi cha ukaidi mwingi, Watoto wasio imani ndani yao.
21 Wamenitia wivu kwa kisicho Mungu; Wamenikasirisha kwa ubatili wao; Nami nitawatia wivu kwa wasio watu, Nami nitawakasirisha kwa taifa lipumbaalo.
22 Maana, moto umewashwa kwa hasira yangu, Unateketea hata chini ya kuzimu, Unakula dunia pamoja na mazao yake, Unaunguza misingi ya milima.
23 Nitaweka madhara juu yao chunguchungu; Nitawapiga kwa mishale yangu hata ikaishe;
24 Watakonda kwa njaa, wataliwa na makaa ya moto, Na uharibifu mkali; Nitawapelekea meno ya wanyama wakali, Pamoja na sumu ya wadudu watambaao mavumbini.
25 Nje upanga utawafifiliza Na ndani ya vyumba, utisho; Utaangamiza mvulana na msichana, Anyonyaye pamoja na mwenye mvi,
26 Nalisema, Ningewatawanyia mbali, Ningekomesha kumbukumbu lao kati ya wanadamu;
27 Isipokuwa naliogopa makamio ya adui, Adui zao wasije wakafikiri uongo, Wasije wakasema, Mkono wetu umetukuka, Wala Bwana hakuyafanya haya yote.
28 Maana hawa ni taifa wasio shauri, Wala fahamu hamna ndani yao.
29 Laiti wangekuwa na akili, hata wakafahamu haya, Ili watafakari mwisho wao.
30 Mmoja angefukuzaje watu elfu, Wawili wangekimbizaje elfu kumi, Kama Mwamba wao asingaliwauza, Kama Bwana asingaliwatoa?
31 Maana, Mwamba wao si kama Mwamba wetu, Hata adui zetu wenyewe ndivyo wahukumuvyo.
32 Maana, mzabibu wao ni mzabibu wa Sodoma, Nao ni wa mashamba ya Gomora; Zabibu zao ni zabibu za uchungu, Vichala vyao ni vichungu.
33 Mvinyo yao ni sumu ya majoka, Uchungu mkali wa nyoka.
34 Je! Haya hayakuwekwa akiba kwangu? Na kutiwa muhuri kati ya hazina yangu?
35 Kisasi ni changu mimi, na kulipa, Wakati itakapoteleza miguu yao; Maana siku ya msiba wao imekaribia, Na mambo yatakayowapata yatafanya haraka.
36 Kwa kuwa Bwana atawaamua watu wake, Atawahurumia watumwa wake, Aonapo ya kuwa nguvu zao zimeondoka, Na ya kuwa habaki mtu, aliyefungwa wala asiyefungwa,
37 Naye atasema, Iko wapi miungu yao, Mwamba ule walioutumaini;
38 Uliokula shahamu za sadaka zao, Na kunywa divai ya sadaka zao za kinywaji? Na waondoke na kuwasaidia ninyi; Na wawe hao himaya yenu.
39 Fahamu sasa ya kuwa Mimi, naam, Mimi ndiye, Wala hapana Mungu mwingine ila Mimi; Naua Mimi, nahuisha Mimi, Nimejeruhi, tena naponya; Wala hapana awezaye kuokoa katika mkono wangu,
40 Maana, nainua mkono wangu mbinguni, Na kusema, Kama Mimi niishivyo milele,
41 Nikiunoa upanga wangu wa umeme, Mkono wangu ukishika hukumu, Nitawatoza kisasi adui zangu, Nitawalipa wanaonichukia.
42 Nitailevya mishale yangu kwa damu, Na upanga wangu utakula nyama; Pamoja na damu ya waliouawa na waliotekwa nyara, Katika vichwa vya wakuu wa adui.
43 Furahini, enyi mataifa, pamoja na watu wake; Kwa maana atatwaa kisasi kwa damu ya watumwa wake, Atawatoza kisasi adui zake, Tena atafanya kafara kwa nchi yake, na watu wake.
44 Musa akaja akasema maneno haya yote ya wimbo huu masikioni mwa watu, yeye na Yoshua, mwana wa Nuni.
45 Musa akamaliza kuwaambia Israeli wote maneno haya yote;
46 akawaambia, Yawekeni mioyoni mwenu maneno yote ambayo nashuhudia kwenu hivi leo; nayo waamuruni watoto wenu, wayatunze na kuyafanya maneno yote ya torati hii.
47 Kwa maana si jambo lisilofaa kwenu; maana, ni maisha yenu, na kwa jambo hili mtazifanya siku zenu kuwa nyingi juu ya nchi mwivukiayo Yordani kuimiliki.
48 Bwana akasema na Musa siku iyo hiyo, akamwambia,
49 Kwea katika mlima huu wa Abarimu, mpaka kilima cha Nebo, kilicho katika nchi ya Moabu, kuelekea Yeriko; ukaangalie nchi ya Kanaani niwapayo wana wa Israeli kuimiliki;
50 ukafe katika kilima, huko ukweako, ukusanywe uwe pamoja na jamaa zako; kama alivyokufa nduguyo Haruni katika mlima wa Hori, akakusanywa awe pamoja na watu wake;
51 kwa sababu mlinikosa ninyi juu yangu katikati ya wana wa Israeli katika maji ya Meriba huko Kadeshi, katika bara ya Sini; kwa kuwa hamkunitakasa katikati ya wana wa Israeli.
52 Kwani utaiona hiyo nchi mbele yako, lakini hutakwenda huko kuingia hiyo nchi niwapayo wana wa Israeli.