0:00
0:00

Mlango 12

Basi hawa ndio wale waliomjia Daudi huko Siklagi, alipokuwa akijificha kwa ajili ya Sauli, mwana wa Kishi; nao walikuwamo miongoni mwa wale mashujaa, waliomsaidia vitani.
2 Walikuwa wenye kupinda upinde, nao walikuwa hodari wa kutumia mkono wa kuume na wa kushoto, kwa kutupa mawe ya teo, na kwa kupiga mishale ya upinde; walikuwa wa nduguze Sauli, wa Benyamini.
3 Mkubwa wao alikuwa Ahiezeri, kisha Yoashi, wana wa Shemaa Mgibeathi; na Yezieli, na Peleti, wana wa Azmawethi; na Beraka, na Yehu Mwanathothi;
4 na Ishmaya Mgibeoni, shujaa wa wale thelathini, naye alikuwa juu ya wale thelathini; na Yeremia, na Yahazieli, na Yohana, na Yozabadi Mgederathi;
5 Eluzai, na Yerimothi, na Bealia, na Shemaria, na Shefatia Mharufi;
6 Elkana, na Ishia, na Azaleli, na Yoezeri, na Yashobeamu, Wakora;
7 na Yoela, na Zebadia, wana wa Yerohamu, wa Gedori.
8 Na wa Wagadi wakajitenga kumfuata Daudi ngomeni huko nyikani, waume mashujaa, watu waliozoea vita, walioweza kutumia ngao na mkuki; ambao nyuso zao zilikuwa kama nyuso za simba, nao walikuwa wepesi kama kulungu juu ya milima;
9 Ezeri mkubwa wao, Obadia wa pili, Eliabu wa tatu;
10 Mishmana wa nne, Yeremia wa tano;
11 Atai wa sita, Elieli wa saba;
12 Yohana wa nane, Elzabadi wa kenda;
13 Yeremia wa kumi, Makbanai wa kumi na moja.
14 Hao wa wana wa Gadi walikuwa maakida wa jeshi, yeye aliyekuwa mdogo amelingana na mia, na yeye aliyekuwa mkuu, na elfu.
15 Hao ndio wale waliovuka Yordani katika mwezi wa kwanza, ulipofurika kingo zake zote; nao wakawakimbiza wote wa bondeni kuelekea mashariki na magharibi pia.
16 Tena wakafika ngomeni kwa Daudi baadhi ya wana wa Benyamini na Yuda.
17 Naye Daudi akatoka ili kuwalaki, akajibu, akawaambia, Kama mmenijia kwa amani ili kunisaidia, basi moyo wangu utaambatana nanyi; lakini kama mmekuja ili kunisaliti kwa adui zangu, kwa kuwa hamna udhalimu mikononi mwangu, Mungu wa baba zetu na alitazame neno hili, na kulikemea.
18 Ndipo roho ikamjilia Abishai, mkuu wa wale thelathini, naye akasema, Sisi tu watu wako, Ee Daudi; Na wa upande wako, Ee mwana wa Yese; Amani, naam, amani iwe kwako, Na amani iwe kwao wakusaidiao; Maana akusaidiye ndiye Mungu wako. Ndipo Daudi akawakaribisha, akawaweka wawe maakida wa kile kikosi.
19 Wa Manase pia wengine walimwangukia Daudi, alipokwenda pamoja na Wafilisti juu ya Sauli vitani, lakini hawakuwasaidia; kwani wale mabwana wa Wafilisti wakafanya shauri, wakamfukuza, wakisema, kwa hatari ya vichwa vyetu atamwangukia bwana wake Sauli.
20 Naye alipokuwa akienda Siklagi, wakamwangukia hawa wa Manase, Adna, na Yozabadi, na Yediaeli, na Mikaeli, na Yozabadi, na Elihu, na Silethai, maakida wa maelfu waliokuwa wa Manase.
21 Wakamsaidia Daudi juu ya kile kikosi kilichomshambulia; kwani walikuwa waume mashujaa wote, nao wakawa maakida jeshini.
22 Maana siku kwa siku humjia Daudi watu wa kumsaidia, hata wakapata kuwa jeshi kubwa, kama jeshi la Mungu.
23 Na hizi ni hesabu za vichwa vya watu wenye silaha za vita, waliokuja Hebroni kwa Daudi, ili kumgeuzia ufalme wa Sauli, sawasawa na neno la Bwana.
24 Wana wa Yuda, waliochukua ngao na mkuki, walikuwa elfu sita na mia nane, wenye silaha za vita.
25 Wa wana wa Simeoni, waume mashujaa wa vita, elfu saba na mia moja.
26 Wa wana wa Lawi, elfu nne na mia sita.
27 Na Yehoyada alikuwa kichwa cha mbari ya Haruni, na pamoja naye walikuwa elfu tatu na mia saba;
28 tena Sadoki, kijana shujaa, na wa nyumba ya babaye, maakida ishirini na wawili.
29 Na wa wana wa Benyamini nduguze Sauli, elfu tatu; kwani hata sasa walio wengi wao walikuwa wameuhifadhi uaminifu wao kwa nyumba ya Sauli.
30 Na wa wana wa Efraimu, ishirini elfu na mia nane, waume mashujaa, watu wenye sifa katika mbari za baba zao.
31 Na wa nusu kabila ya Manase, kumi na nane elfu, waliotajwa majina yao, ili waje kumtawaza Daudi awe mfalme.
32 Na wa wana wa Isakari, watu wenye akili za kujua nyakati, kuyajua yawapasayo Israeli wayatende; vichwa vyao walikuwa watu mia mbili na ndugu zao wote walikuwa chini ya amri yao.
33 Wa Zabuloni, watu wawezao kwenda pamoja na jeshi, hodari wa kupanga vita, wenye zana za vita za kila namna, hamsini elfu; askari wastadi wasiokuwa wenye moyo wa kusita-sita.
34 Na wa Naftali, maakida elfu, na pamoja nao watu wenye ngao na mkuki thelathini na saba elfu.
35 Na wa Wadani, watu hodari wa kupanga vita, ishirini na nane elfu na mia sita.
36 Na wa Asheri, watu wawezao kwenda pamoja na jeshi, hodari wa kupanga vita, arobaini elfu.
37 Tena, ng'ambo ya pili ya Yordani, wa Wareubeni, na wa Wagadi, na wa nusu kabila ya Manase, wenye zana za vita za kupigania za kila namna, mia na ishirini elfu.
38 Hao wote, watu wa vita, askari wastadi, wakaja Hebroni wenye moyo mkamilifu, ili kumtawaza Daudi awe mfalme juu ya Israeli wote; tena wote waliosalia wa Israeli nao walikuwa na moyo mmoja kwamba wamtawaze Daudi.
39 Nao walikuwako huko pamoja na Daudi siku tatu, wakila na kunywa; kwani ndugu zao walikuwa wamewaandalia tayari.
40 Zaidi ya hayo, wale waliokuwa karibu nao, hata mpaka kwa Isakari, na Zabuloni, na Naftali, wakaleta chakula juu ya punda, na ngamia, na nyumbu, na ng'ombe, vyakula vya unga, mikate ya tini, na vichala vya zabibu kavu, na divai, na mafuta, na ng'ombe, na kondoo tele; kwa kuwa kulikuwa na furaha katika Israeli.