0:00
0:00

Mlango 22

Ndipo huyo Elifazi Mtemani akajibu, na kusema,
2 Je! Yumkini mtu awaye yote kumfaa Mungu? Hakika yeye aliye na hekima hujifaa mwenyewe.
3 Je! Mwenyezi hupata furaha katika wewe kuwa mwenye haki? Au je, ni faida kwake, kwamba wafanya njia zako kuwa timilifu?
4 Je! Ni kwa wewe kumcha yeye anakukemea? Na kuingia hukumuni nawe?
5 Je! Uovu wako si mkuu? Wala maovu yako hayana mwisho.
6 Kwa kuwa umetwaa dhamana kwa nduguyo bure, Na kuwavua nguo zao walio uchi.
7 Hukumpa maji ya kunywa huyo aliyechoka, Nawe umemnyima chakula huyo mwenye njaa.
8 Lakini huyo shujaa, nchi ilikuwa yake; Na huyo mwenye kusifiwa, yeye aliikaa.
9 Umewafukuza wanawake wajane hali ya utupu, Na mikono ya mayatima imevunjwa.
10 Kwa hiyo umezungukwa na mitego, Na hofu ya ghafula yakutaabisha,
11 Au je! Huoni giza, Na maji mengi yanayokufunika?
12 Je! Mungu hayuko mbinguni juu? Tena tazama umbali wa nyota, jinsi zilivyo juu!
13 Nawe wasema, Mungu anajua nini? Je! Aweza kuamua kati ya giza kuu?
14 Mawingu mazito ni kifuniko chake, hata asione; Naye yuatembea juu ya kuba ya mbingu.
15 Je! Utaiandama njia ya zamani Waliyoikanyaga watu waovu?
16 Ambao walinyakuliwa kabla ya wakati wao, Msingi wao ulimwagika kama kijito cha maji;
17 Waliomwambia Mungu, Tuondokee; Tena, Huyo Mwenyezi aweza kutufanyia nini?
18 Naye ndiye aliyezijaza nyumba zao vitu vyema; Lakini mashauri ya waovu na yawe mbali nami.
19 Wenye haki huyaona hayo wakafurahi; Nao wasio na hatia huwacheka;
20 Wasema, Hakika hao waliotuinukia wamekatiliwa mbali, Na mabaki yao moto umeyateketeza.
21 Mjue sana Mungu, ili uwe na amani; Ndivyo mema yatakavyokujia.
22 Uyapokee, tafadhali, mafunzo yatokayo kinywani mwake, Na maneno yake yaweke moyoni mwako.
23 Ukimrudia Mwenyezi, utajengwa; Ukiuondoa udhalimu mbali na hema yako.
24 Nawe hazina zako ziweke mchangani, Na dhahabu ya Ofiri iweke kati ya mawe ya vijito;
25 Naye Mwenyezi atakuwa hazina yako, Atakuwa ni fedha ya thamani kwako.
26 Kwani ndipo utakapojifurahisha katika Mwenyezi, Na kuinua uso wako kumwelekea Mungu.
27 Utamwomba yeye naye atakusikia; Nawe utazitimiliza nadhiri zako.
28 Nawe utakusudia neno, nalo litathibitika kwako; Na mwanga utaziangazia njia zako.
29 Hapo watakapokuangusha, utasema, Kuna kuinuka tena; Naye mnyenyekevu Mungu atamwokoa.
30 Atamwokoa na huyo asiye na hatia; Naam, utaokolewa kwa sababu ya usafi wa mikono yako.