0:00
0:00

Mlango 26

Na watu wote wa Yuda wakamtwaa Uzia, naye alikuwa mwenye miaka kumi na sita, wakamfanya awe mfalme mahali pa Amazia babaye.
2 Huyo akajenga Elathi, akaurudisha kwa Yuda, baada ya kulala mfalme pamoja na babaze.
3 Uzia alikuwa na umri wa miaka kumi na sita alipoanza kutawala; akatawala huko Yerusalemu miaka hamsini na miwili; na jina la mamaye aliitwa Yekolia wa Yerusalemu.
4 Akafanya yaliyo ya adili machoni pa Bwana, sawasawa na yote aliyoyafanya Amazia babaye.
5 Akajitia nia amtafute Mungu katika siku za Zekaria, aliyekuwa na fahamu katika maono ya Mungu; na muda alipomtafuta Bwana, Mungu alimfanikisha.
6 Akatoka akapigana na Wafilisti, akauvunja ukuta wa Gathi, na ukuta wa Yabne, na ukuta wa Ashdodi; akajenga miji katika Ashdodi na katikati ya Wafilisti.
7 Mungu akamsaidia juu ya Wafilisti, na juu ya Waarabu waliokaa Gur-baali, na juu ya Wameuni.
8 Na Waamoni wakampa Uzia zawadi; likaenea jina lake mpaka pa kuingilia Misri; kwa kuwa akaongezeka nguvu mno.
9 Tena Uzia akaujengea Yerusalemu minara, penye lango la pembeni, na penye lango la bonde, na ugeukapo ukuta, akaitia nguvu.
10 Akajenga minara tena nyikani, akachimba mabirika mengi, maana alikuwa na ng'ombe tele; katika Shefela pia, na katika nchi tambarare; tena alikuwa na wakulima na watunza mizabibu milimani, na katika mashamba ya neema; maana yeye alipenda ukulima.
11 Zaidi ya hayo Uzia alikuwa na jeshi la watu wa kupigana, waliokwenda vitani vikosi vikosi, sawasawa na hesabu walivyohesabiwa na Yeieli mwandishi, na Maaseya msimamizi, chini ya mkono wa Hanania, mmojawapo wa maakida wa mfalme.
12 Hesabu yote ya wakuu wa nyumba za mababa, watu mashujaa, ilikuwa elfu mbili na mia sita.
13 Na chini ya mkono wao kulikuwa na jeshi la askari, mia tatu na saba elfu, na mia tano, ambao walipigana vita kwa nguvu nyingi, kumsaidia mfalme juu ya adui.
14 Uzia akawafanyizia jeshi lote ngao na mikuki, na chapeo, na deraya za madini, na nyuta, na mawe ya kupiga kwa teo.
15 Akafanya katika Yerusalemu mitambo ya vita, iliyobuniwa na watu wastadi, iwekwe juu ya minara na juu ya buruji, ili kutupa mishale na mawe makubwa. Jina lake likaenea mbali sana; kwa kuwa alisaidiwa mno ajabu, hata akapata nguvu.
16 Lakini alipokuwa na nguvu, moyo wake ulitukuka, hata akafanya maovu, akamwasi Bwana, Mungu wake; kwani aliingia hekaluni mwa Bwana, ili afukize uvumba juu ya madhabahu ya kufukizia.
17 Azaria kuhani akaingia nyuma yake, na pamoja naye makuhani themanini wa Bwana, mashujaa;
18 wakamzuia Uzia mfalme, wakamwambia, Si haki yako, Uzia, kumfukizia Bwana uvumba, ila ni haki ya makuhani wana wa Haruni, waliofanywa wakfu, ili wafukize uvumba; toka katika patakatifu; kwa kuwa umekosa; wala haitakuwa kwa heshima yako kutoka kwa Bwana, Mungu.
19 Akaghadhibika Uzia; naye alikuwa na chetezo mkononi cha kufukizia uvumba; naye hapo alipowaghadhibikia makuhani, ukamtokea ukoma katika paji la uso wake mbele ya makuhani nyumbani mwa Bwana karibu na madhabahu ya kufukizia.
20 Azaria kuhani mkuu na makuhani wote wakamtazama, na angalia, alikuwa na ukoma pajini mwa uso, wakamtoa humo upesi; hata na yeye mwenyewe akafanya haraka kutoka, kwa sababu Bwana amempiga.
21 Uzia mfalme akawa na ukoma hata siku ya kufa kwake, akakaa katika nyumba ya pekee, kwa kuwa ni mwenye ukoma; maana alitengwa na nyumba ya Bwana; na Yothamu mwanawe alikuwa juu ya nyumba ya mfalme, akiwahukumu watu wa nchi.
22 Basi mambo yote ya Uzia yaliyosalia, ya kwanza na ya mwisho, aliyaandika Isaya nabii, mwana wa Amozi.
23 Basi Uzia akalala na babaze; wakamzika pamoja na babaze katika konde la kuzikia la wafalme; kwa kuwa walisema, Huyu ni mwenye ukoma. Na Yothamu mwanawe akatawala mahali pake