0:00
0:00

Mlango 4

Tena akafanya madhabahu ya shaba, mikono ishirini urefu wake, na mikono ishirini upana wake, na mikono kumi kwenda juu kwake.
2 Tena akaifanya bahari ya kusubu, mikono kumi toka ukingo hata ukingo, ya mviringo, na kwenda juu kwake ilikuwa mikono mitano; na uzi wa mikono thelathini kuizunguka kabisa.
3 Na chini yake palikuwa na mifano ya ng'ombe, walioizunguka pande zote ,kwa mikono kumi,wakiizunguka pande zote ile bahari. Ng`ombe walikuwa safu mbili ,wakayeyushwa hapo ilipoyeyushwa hiyo bahari.
4 Ikakaa juu ya ng'ombe kumi na wawili, watatu wakitazama kaskazini, na watatu wakitazama magharibi, na watatu wakitazama kusini, na watatu wakitazama mashariki; na bahari iliwekwa juu yao, na pande zao za nyuma zote zilikuwa ndani.
5 Na unene wake ulikuwa nyanda nne, na ukingo wake ukafanywa kama ukingo wa kikombe, kama ua la yungi; huingia bathi elfu tatu, kukaa ndani yake.
6 Akafanya na birika kumi, akaziweka tano upande wa kuume, na tano upande wa kushoto, za kuoshea; ndizo walizooshea mambo ya kafara; lakini hiyo bahari ilikuwa ya makuhani ya kuogea.
7 Akavifanya vinara vya taa kumi vya dhahabu, kadiri ya vilivyoagiziwa; akavitia hekaluni, vitano upande wa kuume, na vitano upande wa kushoto.
8 Akafanya na meza kumi, akazitia hekaluni, tano upande wa kuume, na tano upande wa kushoto. Kisha akafanya mabakuli mia ya dhahabu.
9 Tena akaufanya ua wa makuhani, na ua mkubwa, nayo milango yake, akaifunikiza kwa shaba milango yake.
10 Nayo bahari akaiweka upande wa kuume kwa mashariki, kuelekea kusini.
11 Na Huramu akayafanya masufuria, na majembe, na mabakuli. Basi Huramu akamaliza kufanya hiyo kazi, aliyomfanyia mfalme Sulemani ya nyumba ya Mungu;
12 zile nguzo mbili, na vimbe, na taji mbili zilizokuwa juu ya nguzo; nazo nyavu mbili za kuzifunika vimbe mbili za taji zilizokuwa juu ya nguzo;
13 na makomamanga mia nne ya nyavu mbili; safu mbili za makomamanga kwa kila wavu, kuzifunika vimbe mbili za taji zilizokuwa juu ya nguzo.
14 Akayafanya na matako, na mabirika akafanya juu ya matako;
15 bahari moja, na ng'ombe kumi na wawili chini yake.
16 Masufuria pia, na majembe, na nyuma, na vyombo vyake vyote, Huramu akamfanyia mfalme Sulemani kwa nyumba ya BWANA ,vya shaba iliyokatuka.
17 Katika uwanda wa Yordani ndipo mfalme alipovisubu, katika udongo mzito kati ya Sukothi na Sereda.
18 Ndivyo alivyovifanya Sulemani vyombo hivyo vyote, vingi sana; kwa kuwa uzani wa shaba ulikuwa hautafutikani.
19 Basi Sulemani akavifanya vyombo vyote vilivyokuwamo nyumbani mwa Mungu, madhabahu ya dhahabu pia, nazo meza, ambazo juu yake iliwekwa mikate ya wonyesho;
20 na vinara na taa zake, ziwake kama ilivyoagizwa mbele ya chumba cha ndani, vya dhahabu iliyosafika;
21 na maua, na taa, na makoleo, ya dhahabu, ndiyo dhahabu bora;
22 na mikasi, na mabakuli, na miiko, na vyetezo, vya dhahabu iliyosafika; na kwa habari za mahali pa kuingia nyumbani, milango yake ya ndani ya patakatifu pa patakatifu, na milango ya nyumba, yaani ya hekalu, ilikuwa ya dhahabu.