0:00
0:00

Mlango 8

Ikawa miaka ishirini ilipopita, ambayo katika hiyo Sulemani aliijenga nyumba ya Bwana, na nyumba yake mwenyewe;
2 ndipo Sulemani akaijenga miji ile Hiramu aliyompa Sulemani, akawakalisha humo wana wa Israeli.
3 Naye Sulemani akaenda Hamath-zoba, akaushinda.
4 Akaujenga Tadmori wa nyikani, na miji yote ya hazina, aliyoijenga katika Hamathi.
5 Tena akaujenga Beth-horoni wa juu, na Beth-horoni wa chini, miji yenye boma, yenye kuta, na malango, na makomeo;
6 na Baalathi, na miji yote ya hazina Sulemani aliyokuwa nayo, na miji yote ya magari yake, na miji ya wapanda farasi wake, na ya anasa yote aliyopenda Sulemani kujenga humo Yerusalemu, na katika Lebanoni, na katika nchi yote ya mamlaka yake.
7 Basi kwa habari ya watu wote waliosalia wa Wahiti, na wa Waamori, na wa Waperizi, na wa Wahivi, na wa Wayebusi, wasiokuwa wa Israeli;
8 wa watoto wao waliosalia baada yao katika nchi, ambao wana wa Israeli hawakuwakomesha, katika hao Sulemani akawatumikisha shokoa hata leo.
9 Wala katika wana wa Israeli Sulemani hakuwafanya watumwa kazini mwake; lakini hao walikuwa watu wa vita, na wakuu wa majemadari wake, na maakida wa magari yake na wa wapanda farasi wake.
10 Na hao walikuwa maakida wakuu wa Sulemani, watu mia mbili na hamsini, waliotawala juu ya watu.
11 Sulemani akamleta binti Farao kutoka mji wa Daudi mpaka nyumba aliyomjengea; kwa kuwa alisema, Mke wangu hatakaa nyumbani mwa Daudi mfalme wa Israeli, kwa kuwa ni patakatifu, mahali palipofika sanduku la Bwana.
12 Ndipo Sulemani akamtolea Bwana sadaka za kuteketezwa juu ya madhabahu ya Bwana, aliyoijenga mbele ya ukumbi,
13 kadiri ilivyohitajiwa huduma ya kila siku, akitoa sawasawa na amri ya Musa, siku za sabato, na za mwezi mpya, na za sikukuu zilizoamriwa, mara tatu kila mwaka, yaani, sikukuu ya mikate isiyochachwa, na sikukuu ya majuma, na sikukuu ya vibanda.
14 Akaziamuru, sawasawa na agizo la Daudi babaye, zamu za makuhani za kutumika, nao Walawi kwa kadiri ya malinzi yao, ili kusifu, na kuhudumu mbele ya makuhani, kama ilivyohitajiwa kila siku; tena mabawabu kwa zamu zao za kila mlango; maana ndivyo alivyoamuru Daudi mtu wa Mungu.
15 Wala hawakuyaacha maagizo ya mfalme aliyowaamuru makuhani na Walawi kwa neno lo lote, wala kwa habari ya hazina.
16 Basi ikatengenezwa kazi yote ya Sulemani hata siku ya kutiwa msingi wa nyumba ya Bwana, na hata ilipokwisha. Hivyo ikamalizika nyumba ya Bwana.
17 Ndipo Sulemani akaenda Esion-geberi, na Elothi, pwani ya nchi ya Edomu.
18 Naye Hiramu akamletea merikebu kwa mikono ya watumishi wake, na watumishi waliokuwa wana-maji; nao wakafika Ofiri pamoja na watumishi wa Sulemani, wakachukua kutoka huko talanta mia nne na hamsini za dhahabu, wakamletea mfalme Sulemani.