0:00
0:00

Mlango 18

Ole wa nchi ya uvumi wa mabawa, Iliyoko mbali kupita mito ya Kushi;
2 Ipelekayo wajumbe wake kwa njia ya bahari, Na katika vyombo vya manyasi juu ya maji. Nendeni, wajumbe wepesi,kwa watu warefu,laini; Watu watishao tangu mwanzo wao hata sasa; Taifa la wenye nguvu,wakanyagao watu, Ambao mito inakata nchi yao.
3 Enyi watu mkaao katika ulimwengu wote, na wenyeji wa dunia, bendera ikiinuliwa milimani, angalieni; na wakipiga tarumbeta, sikieni.
4 Maana Bwana ameniambia hivi, Mimi nitatulia, na kuangalia katika makazi yangu, kama wakati wa mwangaza mweupe wa jua kali, mfano wa wingu la umande katika hari ya mavuno.
5 Maana kabla ya mavuno, maua yaangukapo, na maua yakawa zabibu zianzazo kuiva, ndipo atakapoyakata matawi kwa miundu, na kuviondoa vitawi vilivyopanuka na kuvikata.
6 Wote pamoja wataachiwa ndege wakali wa milimani, na hayawani wa nchi; ndege wakali watakaa juu yao wakati wa jua, na hayawani wote wa nchi watakaa juu yao wakati wa baridi.
7 Wakati huo Bwana wa majeshi ataletewa hedaya na watu warefu, laini; Watu watishao tangu mwanzo wao hata sasa; Taifa la wenye nguvu, wakanyagao watu, Ambao mito inakata nchi yao; mpaka mahali pa jina la Bwana wa majeshi,mlima Sayuni.