0:00
0:00

Mlango 51

Nisikilizeni, ninyi mnaoifuatia haki; ninyi mnaomtafuta Bwana; uangalieni mwamba ule ambao mlitolewa kwa kuchongwa, na tundu la shimo ambalo mlitolewa kwa kuchimbuliwa.
2 Mwangalieni Ibrahimu, baba yenu, na Sara, aliyewazaa; kwa maana alipokuwa mmoja tu nalimwita, nikambariki, nikamfanya kuwa wengi.
3 Maana Bwana ameufariji Sayuni; amepafariji mahali pake palipokuwa ukiwa; amefanya jangwa lake kuwa kama bustani ya Edeni, na nyika yake kama bustani ya Bwana; furaha na kicheko zitaonekana ndani yake, kushukuru, na sauti ya kuimba.
4 Nisikilizeni mimi, enyi watu wangu; nisikieni, taifa langu; maana sheria itatoka kwangu, nami nitaistarehesha hukumu yangu iwe nuru ya mataifa.
5 Haki yangu i karibu, wokovu wangu umekuwa wazi, na mikono yangu itawahukumu kabila za watu; visiwa vitaningoja, navyo vitautumainia mkono wangu.
6 Inueni macho yenu mbinguni, mkaitazame nchi chini; maana mbingu zitatoweka kama moshi, na nchi itachakaa kama vazi, nao wakaao ndani yake watakufa kadhalika; bali wokovu wangu utakuwa wa milele, na haki yangu haitatanguka.
7 Nisikilizeni, ninyi mjuao haki, watu ambao mioyoni mwenu mna sheria yangu; msiogope matukano ya watu, wala msifadhaike kwa sababu ya dhihaka zao.
8 Maana nondo itawala kama vazi, na funza atawala kama sufu; bali haki yangu itakuwa ya milele, na wokovu wangu hata vizazi vyote.
9 Amka, amka, jivike nguvu, Ee mkono wa Bwana; Amka kama katika siku zile za kale, Katika vizazi vile vya zamani.
10 Si wewe uliyemkata-kata Rahabu? Uliyemchoma yule joka? Si wewe uliyeikausha bahari, Na maji ya vilindi vikuu; Uliyevifanya vilindi kuwa njia, Ili wapite watu waliokombolewa?
11 Nao waliokombolewa na Bwana watarejea, Watafika Sayuni, wakiimba; Furaha ya milele itakuwa juu ya vichwa vyao; Watapata shangwe na furaha; Huzuni na kuugua zitakimbia.
12 Mimi, naam, mimi, ndimi niwafarijiye; wewe u nani hata ukamwogopa mtu atakayekufa, na mwanadamu atakayefanywa kuwa kama majani?
13 Ukamsahau Bwana, Muumba wako, yeye aliyezitanda mbingu, na kuiweka misingi ya dunia; nawe unaogopa daima mchana kutwa kwa sababu ya ghadhabu yake yeye aoneaye, hapo afanyapo tayari kuharibu; nayo i wapi ghadhabu yake aoneaye?
14 Yeye aliyehamishwa na kufungwa atafunguliwa kwa haraka; wala hatakufa na kushuka shimoni, wala chakula chake hakitapunguka.
15 Maana mimi ni Bwana, Mungu wako, niichafuaye bahari, mawimbi yake yakavuma.
16 Bwana wa majeshi ndilo jina lake. Nami nimetia maneno yangu kinywani mwako, nami nimekusitiri katika kivuli cha mkono wangu, ili nizipande mbingu, na kuiweka misingi ya dunia, na kuuambia Sayuni, Ninyi ni watu wangu.
17 Amka, amka, simama, Ee Yerusalemu, Wewe uliyenywea, mkononi mwa Bwana, Kikombe cha hasira yake; Bakuli la kikombe cha kulevya-levya Umelinywea na kulimaliza.
18 Hapana hata mmoja wa kumwongoza Miongoni mwa wana wote aliowazaa, Wala hapana hata mmoja wa kumshika mkono Miongoni mwa wana wote aliowalea.
19 Mambo haya mawili yamekupata; Ni nani awezaye kukusikitikia? Ukiwa na uharibifu, na njaa na upanga; Niwezeje kukutuliza?
20 Wana wako wamezimia, Wamelala penye pembe za njia kuu zote Kama kulungu wavuni; Wamejaa hasira ya Bwana, Lawama ya Mungu wako.
21 Basi, kwa sababu ya hayo, ulisikilize neno hili, ewe uliyeteswa, na kulewa, lakini si kwa mvinyo;
22 Bwana, Bwana wako na Mungu wako, awateteaye watu wake, asema hivi, Tazama, nimeondoa mkononi mwako kikombe cha kulevya-levya, hilo bakuli la kikombe cha hasira yangu; hutakinywea tena;
23 nami nitakitia mikononi mwao wakutesao; waliokuambia nafsi yako, Inama, tupate kupita; nawe uliufanya mgongo wako kuwa kama nchi, na kama njia, kwa hao wapitao juu yake.