0:00
0:00

Mlango 63

Ni nani huyu atokaye Edomu, Mwenye mavazi ya kutiwa damu kutoka Bosra? Huyu aliye na nguo za fahari, Anayekwenda katika ukuu wa uweza wake?
2 Kwani mavazi yako kuwa mekundu, Na nguo zako kama za mtu akanyagaye zabibu?
3 Nalikanyaga shinikizoni peke yangu; Wala katika watu hakuwapo mtu pamoja nami; Naam, naliwakanyaga kwa hasira yangu, Naliwaponda kwa ghadhabu yangu; Na mavazi yangu yametiwa madoa kwa damu yao, Nami nimezichafua nguo zangu zote.
4 Maana siku ya kisasi ilikuwamo moyoni mwangu, Na mwaka wao niliowakomboa umewadia.
5 Nikatazama, wala hakuna wa kusaidia; Nikashangaa kwa kuwa hakuna mwenye kutegemeza; Basi, mkono wangu mwenyewe uliniletea wokovu, Ghadhabu yangu ndiyo iliyonitegemeza.
6 Nikazikanyaga kabila za watu kwa hasira yangu, Nikawalevya kwa ghadhabu yangu, Nami nikaimwaga damu yao chini.
7 Nitautaja wema wa Bwana, sifa za Bwana kwa yote aliyotukirimia Bwana; na wingi wa wema wake kwa nyumba ya Israeli, aliowakirimia kwa rehema zake, na kwa wingi wa wema wake.
8 Maana alisema, Hakika ndio watu wangu hawa, wana wasio na hila; akawa Mwokozi wao.
9 Katika mateso yao yote yeye aliteswa, na malaika wa uso wake akawaokoa; kwa mapenzi yake, na huruma zake, aliwakomboa mwenyewe; akawainua, akawachukua siku zote za kale.
10 Lakini wakaasi, wakamhuzunisha Roho yake Mtakatifu; kwa hiyo akawageukia, akawa adui, akapigana nao.
11 Ndipo alipozikumbuka siku za kale, za Musa, na watu wake, akisema, Yuko wapi yeye aliyewapandisha toka baharini pamoja na wachungaji wa kundi lake? Yuko wapi yeye aliyetia kati yao Roho yake Mtakatifu?
12 Aliyewaongoza kwa mkono wake mtukufu, kwa mkono wa kuume wa Musa? Aliyeyatenga maji mbele yao, ili ajifanyie jina la milele?
13 Aliyewaongoza vilindini, kama farasi jangwani, wasijikwae?
14 Kama ng'ombe washukao bondeni, Roho ya Bwana akawastarehesha; ndivyo ulivyowaongoza watu wako, ili ujifanyie jina lenye utukufu.
15 Tazama toka mbinguni, ukaone toka makao ya utukufu wako na fahari yako; uko wapi wivu wako, na uweza wako? Shauku ya moyo wako, na huruma zako zimezuiliwa kwangu.
16 Maana wewe ndiwe Baba yetu, ijapokuwa Ibrahimu hatujui, wala Israeli hatukiri; wewe, Bwana, ndiwe Baba yetu, mkombozi wetu tangu milele ndilo jina lako.
17 Ee Bwana, mbona umetukosesha njia zako, ukatufanyiza kuwa na mioyo migumu hata tusikuogope? Urudi kwa ajili ya watumishi wako, kabila za urithi wako.
18 Watu wako watakatifu waliumiliki kwa kitambo tu; adui zetu wamepakanyaga patakatifu pako.
19 Tumekuwa kama watu usiowamiliki kamwe; kama watu wasioitwa kwa Jina lako.