0:00
0:00

Mlango 39

Wakati huo Merodaki-baladani, mwana wa Baladani, mfalme wa Babeli, alipeleka barua na zawadi kwa Hezekia; kwa maana amepata habari kwamba amekuwa hawezi, na kwamba amepona.
2 Hezekia akawafurahia, akawaonyesha nyumba yake yenye vitu vyake vya thamani, fedha na dhahabu, na manukato, na marhamu ya thamani, na nyumba yote yenye silaha zake za vita, na vitu vyote vilivyoonekana katika hazina zake; hapakuwa na kitu nyumbani mwake wala katika ufalme wake asichowaonyesha.
3 Ndipo Isaya nabii akamwendea mfalme Hezekia, akamwambia, Watu hawa walisema nini? Nao wametoka wapi kuja kwako? Hezekia akasema, Wametoka katika nchi iliyo mbali, wakaja kwangu toka Babeli.
4 Ndipo akasema, Wameona nini katika nyumba yako? Hezekia akajibu, Wameviona vitu vyote vilivyomo nyumbani mwangu; hapana kitu katika hazina zangu nisichowaonyesha.
5 Ndipo Isaya akamwambia Hezekia, Basi, lisikie neno la Bwana wa majeshi.
6 Tazama, siku zinakuja, ambazo vitu vyote vilivyomo nyumbani mwako, na hivyo vilivyowekwa akiba na baba zako hata leo, vitachukuliwa mpaka Babeli; hapana kitu cho chote kitakachosalia; asema Bwana.
7 Na baadhi ya wana wako utakaowazaa, watakaotoka kwako, watawachukulia mbali; nao watakuwa matowashi katika jumba la mfalme wa Babeli.
8 Ndipo Hezekia akamwambia Isaya, Neno la Bwana ulilolinena ni jema. Tena akamwambia, Maana itakuwapo amani na kweli katika siku zangu mimi.