0:00
0:00

Mlango 7

Hata ikawa katika siku za Ahazi, mwana wa Yothamu, mwana wa Uzia, mfalme wa Yuda, Resini, mfalme wa Shamu, na Peka, mwana wa Remalia, mfalme wa Israeli, wakapanda wakaenda Yerusalemu ili kupigana nao, lakini hawakuweza kuushinda.
2 Kisha watu wa nyumba ya Daudi wakaambiwa kwamba Shamu wamefanya mapatano na Efraimu. Na moyo wake ukataharuki, na moyo wa watu wake, kama miti ya mwituni itikiswavyo na upepo.
3 Basi Bwana akamwambia Isaya, Haya, toka, umlaki Ahazi, wewe na Shear-yashubu mwana wako, huko mwisho wa mfereji wa birika la juu, katika njia kuu ya uwanja wa dobi;
4 ukamwambie, Angalia, ukatulie; usiogope wala usife moyo, kwa sababu ya mikia hii miwili ya vinga hivi vitokavyo moshi; kwa sababu ya hasira kali ya Resini na Shamu, na mwana wa Remalia.
5 Kwa kuwa Shamu amekusudia mabaya juu yako, pamoja na Efraimu na mwana wa Remalia, wakisema,
6 Haya, na tupande ili kupigana na Yuda na kuwasumbua, tukabomoe mahali tupate kuingia, na kummilikisha mfalme ndani yake, huyo mwana wa Tabeeli.
7 Bwana MUNGU asema hivi, Neno hili halitasimama wala halitakuwa.
8 Kwa maana kichwa cha Shamu ni Dameski, na kichwa cha Dameski ni Resini; na katika muda wa miaka sitini na mitano Efraimu atavunjika vipande vipande, asiwe kabila ya watu tena;
9 tena kichwa cha Efraimu ni Samaria, na kichwa cha Samaria ni mwana wa Remalia. Kwamba hamtaki kusadiki, bila shaka hamtathibitika.
10 Tena Bwana akasema na Ahazi akinena,
11 Jitakie ishara ya Bwana, Mungu wako; itake katika mahali palipo chini sana, au katika mahali palipo juu sana.
12 Lakini Ahazi akasema, Sitaitaka, wala sitamjaribu Bwana.
13 Naye akasema, Sikilizeni sasa, enyi nyumba ya Daudi; Je! Ni neno dogo kwenu kuwachosha wanadamu, hata mkataka kumchosha Mungu wangu pia?
14 Kwa hiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara. Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa mtoto mwanamume, naye atamwita jina lake Imanueli.
15 Siagi na asali atakula, wakati ajuapo kuyakataa mabaya na kuyachagua mema.
16 Kwa maana kabla mtoto huyo hajajua kuyakataa mabaya na kuyachagua mema, nchi ile, ambayo wewe unawachukia wafalme wake wawili, itaachwa ukiwa.
17 Bwana ataleta juu yako, na juu ya watu wako, na juu ya nyumba ya baba yako, siku zisizokuja bado, tangu siku ile aliyoondoka Efraimu kutoka katika Yuda; yaani, mfalme wa Ashuru.
18 Tena itakuwa katika siku hiyo Bwana atampigia kelele inzi aliye katika pande za mwisho za mito ya Misri, na nyuki aliye katika nchi ya Ashuru
19 Nao watakuja na kutulia katika mabonde yaliyo ukiwa, na katika pango za majabali, na juu ya michongoma yote, na juu ya malisho yote.
20 Katika siku hiyo Bwana atanyoa kichwa na malaika ya miguuni, kwa wembe ulioajiriwa pande za ng'ambo ya Mto, yaani, kwa mfalme wa Ashuru, nao utazimaliza ndevu nazo.
21 Katika siku hiyo itakuwa ya kwamba mtu atalisha ng'ombe mke mchanga na kondoo wake wawili;
22 kisha itakuwa, kwa sababu wanyama hao watatoa maziwa mengi, atakula siagi; kwa maana kila mtu aliyesalia katika nchi hii atakula siagi na asali.
23 Tena itakuwa katika siku hiyo kila mahali palipokuwa na mizabibu elfu, iliyopata fedha elfu, patakuwa mahali pa mbigili na miiba tu.
24 Mtu atakayekwenda huko atakwenda na mishale na upinde; kwa sababu nchi yote itakuwa ina mibigili na miiba.
25 Na vilima vyote vilivyolimwa kwa jembe, hutafika huko kwa sababu ya kuiogopa mibigili na miiba, lakini hapo patakuwa mahali pa kupeleka ng'ombe, mahali pa kukanyagwa na kondoo.