0:00
0:00

Mlango 60

Ondoka, uangaze; kwa kuwa nuru yako imekuja, Na utukufu wa Bwana umekuzukia.
2 Maana, tazama, giza litaifunika dunia, Na giza kuu litazifunika kabila za watu; Bali Bwana atakuzukia wewe, Na utukufu wake utaonekana juu yako.
3 Na mataifa wataijilia nuru yako, Na wafalme kuujia mwanga wa kuzuka kwako.
4 Inua macho yako, utazame pande zote; Wote wanakusanyana; wanakujia wewe; Wana wako watakuja kutoka mbali. Na binti zako watabebwa nyongani.
5 Ndipo utakapoona na kutiwa nuru, Na moyo wako utatetemeka na kukunjuka; Kwa kuwa wingi wa bahari utageuzwa kukujia, Utajiri wa mataifa utakuwasilia.
6 Wingi wa ngamia utakufunika, Ngamia vijana wa Midiani na Efa; Wote watakuja kutoka Sheba; Wataleta dhahabu na uvumba; Na kuzitangaza sifa za Bwana.
7 Makundi yote ya Kedari yatakusanyika kwako, Kondoo waume wa Nebayothi watakutumikia; Watapanda juu ya madhabahu yangu kwa kibali, Nami nitaitukuza nyumba ya utukufu wangu.
8 Ni nani hawa warukao kama wingu, Na kama njiwa waendao madirishani kwao?
9 Hakika yake visiwa vitaningojea, Na merikebu za Tarshishi kwanza, Ili kuleta wana wako kutoka mbali, Na fedha yao na dhahabu yao pamoja nao, Kwa ajili ya jina la Bwana, Mungu wako, Kwa ajili yake Mtakatifu wa Israeli, Kwa kuwa amekutukuza wewe.
10 Na wageni watajenga kuta zako, Na wafalme wao watakuhudumu; Maana katika ghadhabu yangu nalikupiga, Lakini katika upendeleo wangu nimekurehemu.
11 Malango yako nayo yatakuwa wazi daima; Hayatafungwa mchana wala usiku; Ili watu wapate kukuletea utajiri wa mataifa, Na wafalme wao wakiongozwa pamoja nao.
12 Kwa maana kila taifa na ufalme wa watu Wasiotaka kukutumikia wataangamia; Naam, mataifa hayo wataharibiwa kabisa.
13 Utukufu wa Lebanoni utakujia wewe, Mberoshi na mtidhari na mteashuri pamoja; Ili kupapamba mahali pangu patakatifu, Nami nitapatukuza mahali pa miguu yangu.
14 Na wana wa watu wale waliokutesa Watakuja kwako na kukuinamia; Nao wote waliokudharau Watajiinamisha hata nyayo za miguu yako; Nao watakuita, Mji wa Bwana, Sayuni wa Mtakatifu wa Israeli.
15 Na kwa kuwa umeachwa na kuchukiwa, Hata ikawa hapana mtu aliyepita ndani yako, Nitakufanya kuwa fahari ya milele, Furaha ya vizazi vingi.
16 Utanyonya maziwa ya mataifa, Utanyonya matiti ya wafalme; Nawe utajua ya kuwa mimi, Bwana, ni mwokozi wako, Na mkombozi wako, Mwenye enzi wa Yakobo.
17 Badala ya shaba nitaleta dhahabu, Na badala; ya chuma nitaleta fedha, Na badala ya mti, shaba, Na badala ya mawe, chuma; Tena nitawafanya wasimamizi wako wawe amani, Na hao wakutozao fedha kuwa haki.
18 Jeuri haitasikiwa tena katika nchi yako, Ukiwa na uharibifu hazitakuwa mipakani mwako; Bali utaziita kuta zako, Wokovu, Na malango yako, Sifa.
19 Jua halitakuwa nuru yako tena wakati wa mchana, Wala mwezi hautakupa nuru kwa mwangaza wake; Bali Bwana atakuwa nuru ya milele kwako, Na Mungu wako atakuwa utukufu wako.
20 Jua lako halitashuka tena, Wala mwezi wako hautajitenga; Kwa kuwa Bwana mwenyewe atakuwa nuru yako ya milele; Na siku za kuomboleza kwako zitakoma.
21 Watu wako nao watakuwa wenye haki wote, Nao watairithi nchi milele;
22 Mdogo atakuwa elfu, Na mnyonge atakuwa taifa hodari; Mimi, Bwana, nitayahimiza hayo wakati wake.