0:00
0:00

Mlango 66

Bwana asema hivi, Mbingu ni kiti changu cha enzi, na dunia ni mahali pa kuweka miguu yangu; mtanijengea nyumba ya namna gani? Na mahali pangu pa kupumzikia ni mahali gani?
2 Maana mkono wangu ndio uliofanya hivi vyote, vitu hivi vyote vikapata kutokea, asema Bwana; lakini mtu huyu ndiye nitakayemwangalia, mtu aliye mnyonge, mwenye roho iliyopondeka, atetemekaye asikiapo neno langu.
3 Yeye achinjaye ng'ombe ni kama yeye amwuaye mtu; na yeye atoaye dhabihu ya mwana-kondoo ni kama yeye avunjaye shingo ya mbwa; na yeye atoaye matoleo ni kama yeye atoaye damu ya nguruwe; na yeye afukizaye uvumba ni kama yeye abarikiye sanamu; naam, wamezichagua njia zao wenyewe, na nafsi zao zafurahia machukizo yao.
4 Mimi nami nitachagua mapigo yao, nitaleta hofu zao juu yao; kwa sababu nilipoita, hawakuitika; na niliponena, hawakusikia; bali walifanya yaliyo maovu machoni pangu, na kuyachagua nisiyoyafurahia.
5 Lisikilizeni neno la Bwana, ninyi mtetemekao kwa sababu ya neno lake; Ndugu zenu wawachukiao ninyi, waliowatupa kwa ajili ya jina langu, wamesema, Na atukuzwe Bwana, tupate kuiona furaha yenu; lakini watatahayarika.
6 Sauti ya fujo itokayo mjini! Sauti itokayo hekaluni! Sauti ya Bwana awalipaye adui zake adhabu!
7 Kabla hajaona utungu alizaa; Kabla maumivu yake hayajampata, Alizaa mtoto mwanamume.
8 Ni nani aliyesikia neno kama hili? Ni nani aliyeona mambo kama haya? Je! Nchi yaweza kuzaliwa siku moja? Taifa laweza kuzaliwa mara? Maana Sayuni, mara alipoona utungu, Alizaa watoto wake.
9 Je! Mimi nilete wana karibu na kuzaliwa, nisizalishe? Asema Bwana; mimi nizalishaye, je! Nilifunge tumbo? Asema Mungu wako.
10 Furahini pamoja na Yerusalemu, shangilieni kwa ajili yake, ninyi nyote mmpendao; furahini pamoja naye kwa furaha, ninyi nyote mliao kwa ajili yake;
11 mpate kunyonya, na kushibishwa kwa maziwa ya faraja zake, mpate kukama, na kufurahiwa kwa wingi wa utukufu wake.
12 Maana Bwana asema hivi, Tazama, nitamwelekezea amani kama mto, na utukufu wa mataifa kama kijito kifurikacho, nanyi mtapata kunyonya; mtabebwa; na juu ya magoti mtabembelezwa.
13 Mfano wa mtu ambaye mama yake amfariji, ndivyo nitakavyowafariji ninyi; nanyi mtafarijiwa katika Yerusalemu.
14 Nanyi mtaona, na mioyo yenu itafurahi, na mifupa yenu itasitawi kama majani mabichi; na mkono wa Bwana utajulikana, uwaelekeao watumishi wake, naye atawaonea adui zake ghadhabu.
15 Maana Bwana atakuja na moto, na magari yake ya vita kama upepo wa kisulisuli; ili atoe malipo ya ghadhabu yake kwa moto uwakao, na maonyo yake kwa miali ya moto.
16 Kwa maana Bwana atateta na wote wenye mwili, kwa moto na kwa upanga wake; nao watakaouawa na Bwana watakuwa wengi.
17 Watu wale wajitakasao, na kujisafisha katika bustani, nyuma yake aliye katikati; wakila nyama ya nguruwe, na machukizo, na panya; watakoma pamoja, asema Bwana.
18 Nami nayajua matendo yao na mawazo yao; wakati unakuja nitakapokusanya mataifa yote na lugha zote; nao watakuja, nao watauona utukufu wangu.
19 Nami nitaweka ishara kati yao, nami nitawatuma hao waliookoka kwa mataifa, Tarshishi, na Puli, na Ludi, wavutao upinde, kwa Tubali na Yavani, visiwa vilivyo mbali; watu wasioisikia habari yangu, wala kuuona utukufu wangu; nao watahubiri utukufu wangu katika mataifa.
20 Nao watawaleta ndugu zenu wote kutoka mataifa yote, kuwa sadaka kwa Bwana, juu ya farasi, na katika magari, na katika machela, na juu ya nyumbu, na juu ya wanyama wepesi, mpaka mlima wangu mtakatifu Yerusalemu, asema Bwana; kama vile wana wa Israeli waletavyo sadaka yao nyumbani kwa Bwana katika chombo safi.
21 Na baadhi ya hao nitawatwaa kuwa makuhani na Walawi, asema Bwana.
22 Kama vile mbingu mpya na nchi mpya, nitakazofanya, zitakavyokaa mbele zangu, asema Bwana, ndivyo uzao wenu na jina lenu litakavyokaa.
23 Na itakuwa, mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato, wanadamu wote watakuja kuabudu mbele zangu, asema Bwana.
24 Nao watatoka nje na kuitazama mizoga ya watu walioniasi; maana funza wao hatakufa, wala moto wao hautazimika nao watakuwa chukizo machoni pa wote wenye mwili.