0:00
0:00

Mlango 52

Amka, amka, jivike nguvu zako, Ee Sayuni; Jivike mavazi yako mazuri, Ee Yerusalemu, mji mtakatifu; Kwa maana tokea sasa hataingia ndani yako Asiyetahiriwa, wala aliye najisi.
2 Jikung'ute mavumbi; uondoke, Uketi, Ee Yerusalemu; Jifungulie vifungo vya shingo yako, Ee binti Sayuni uliyefungwa.
3 Maana Bwana asema hivi, Mliuzwa bure; nanyi mtakombolewa bila fedha.
4 Maana Bwana MUNGU asema hivi, Watu wangu hapo kwanza walishuka Misri ili wakae huko hali ya ugeni; na Mwashuri akawaonea bila sababu.
5 Basi sasa, nafanya nini hapa, asema Bwana, ikiwa watu wangu wamechukuliwa bure? Hao wanaowatawala wanapiga yowe, asema Bwana, na jina langu linatukanwa daima mchana kutwa.
6 Kwa hiyo watu wangu watalijua jina langu kwa hiyo watajua siku ile ya kuwa mimi ndimi ninenaye; tazama ni mimi.
7 Jinsi ilivyo mizuri juu ya milima Miguu yake aletaye habari njema, Yeye aitangazaye amani, Aletaye habari njema ya mambo mema, Yeye autangazaye wokovu, Auambiaye Sayuni, Mungu wako anamiliki!
8 Sauti ya walinzi wako! Wanapaza sauti zao, wanaimba pamoja; Maana wataona jicho kwa jicho, Jinsi Bwana arejeavyo Sayuni.
9 Pigeni kelele za furaha, imbeni pamoja, Enyi mahali pa Yerusalemu palipokuwa ukiwa; Kwa kuwa Bwana amewafariji watu wake, Ameukomboa Yerusalemu.
10 Bwana ameweka wazi mkono wake mtakatifu Machoni pa mataifa yote; Na ncha zote za dunia Zitauona wokovu wa Mungu wetu.
11 Nendeni zenu, nendeni zenu, tokeni huko, msiguse kitu kichafu; tokeni kati yake; iweni safi ninyi mnaochukua vyombo vya Bwana.
12 Maana hamtatoka kwa haraka, wala hamtakwenda kwa kukimbia, kwa sababu Bwana atawatangulia; na Mungu wa Israeli atawafuata nyuma; awalinde.
13 Tazama, mtumishi wangu atatenda kwa busara, atatukuzwa, na kuinuliwa juu, naye atakuwa juu sana.
14 Kama vile wengi walivyokustaajabia, (uso wake ulikuwa umeharibiwa sana zaidi ya mtu ye yote, na umbo lake zaidi ya wanadamu),
15 ndivyo atakavyowasitusha mataifa mengi; wafalme watamfumbia vinywa vyao; maana mambo wasiyoambiwa watayaona; na mambo wasiyoyasikia watayafahamu.